Rais Samia: “Serikali Ipo Tayari Kukabiliana na Jaribio Lolote la Kuchochea Machafuko”

 

Rais Samia Suluhu Hassan amesema kuwa serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya jaribio lolote la kuendeleza maandamano au machafuko nchini, akibainisha kuwa taarifa za kiintelijensia zinaonesha baadhi ya waandaaji wa vurugu wamekuwa wakibadili tarehe za mipango yao.

Akizungumza na Wazee wa Jiji Dar es Salaam, Rais Samia alifichua kuwa mmoja wa wahusika wa mpango huo ameshauri kikundi chake kuepuka tarehe 9 Desemba na badala yake kuelekeza maandamano yao tarehe 25 Desemba.

“Nataka niwaambie, wakati wowote wakija—tumejipanga,” alisema Rais Samia.

Amesema baadhi ya watu wamekuwa wakituma ujumbe serikalini wakitoa masharti ya kufanya mazungumzo, lakini akasisitiza kuwa serikali haitalazimishwa kuchukua maamuzi kinyume na misingi ya uhuru wa taifa.

“Serikali hii haiwezi kuamrishwa. Sisi ni nchi huru,” aliongeza.

Katika kuelezea presha kutoka kwa baadhi ya makundi, Rais Samia amesema kumekuwa na shinikizo la “kumuachia mtu fulani” kama sehemu ya masharti ya maridhiano. Hata hivyo, amesema maridhiano ya kweli hayawezi kujengwa juu ya mashinikizo kutoka nje bali kupitia utashi wa Watanzania wenyewe.

Akimnukuu ushindi wa CCM katika uchaguzi uliopita, ambao aliusema uliifikia asilimia 97, Rais Samia aliwajibu wanaohoji kiwango hicho akisema:

“Wanaouliza kwa nini asilimia hiyo ni kubwa, hawakuwepo kwenye uchaguzi. Hawapaswi kutilia shaka maamuzi ya waliojitokeza kupiga kura.”

Ametumia nafasi hiyo kuhimiza umuhimu wa majadiliano na mshikamano wa kitaifa, akisisitiza kuwa licha ya majeraha ya kisiasa yaliyowahi kutokea, Watanzania wenyewe ndiyo wenye uwezo wa kuyaweka sawa kupitia majukwaa ya mazungumzo, hekima za wazee, na kuwaongoza vijana kutoshirikishwa katika mipango ya uchochezi.

“Tukae tuzungumze. Wazee wetu na vijana wetu wasitumike. Tanzania itajengwa na Watanzania,” amehitimisha.

Chapisha Maoni

0 Maoni