Wachambuzi wa masuala ya siasa, diplomasia, na
maendeleo wametoa wito kwa vijana na wananchi kwa ujumla kutumia mitandao ya
kijamii kwa busara na uzalendo, huku wakisisitiza umuhimu wa kufanya tathmini
ya kina kuhusu ukweli wa taarifa wanazopokea na kusambaza, hususan katika
kipindi hiki kuelekea uchaguzi.
Wito huo umetolewa Oktoba 26, 2025, jijini Dar es
Salaam, wakati wa mdahalo wa 'Wajibu wa Kidijitali kwa Amani ya Nchi Kabla,
Wakati na Baada ya Uchaguzi” uliofanyika katika Ukumbi wa American Corner,
Makumbusho ya Taifa.
Akifungua mdahalo huo Mwenyekiti wa Jukwaa la Wachambuzi
Maggid Mjengwa alitahadharisha kuhusu athari za machafuko na kueleza kuwa
watakao athirika zaidi ni wananchi masikini ambao ndio wengi kwani wenye uwezo baadhi
yao wengine watoto wao wapo nje ya nchi.
Mjengwa ametoa mfano wa wakimbizi wa nchi ya Sudan
waliopo Tanzania ambao wengi wao wanasomea udaktari, ambapo amesema wazazi wao
wote wanauwezo na wamewapangia nyumba maeneo mazuri tu kama Masaki, huku watoto
wa masikini wa Sudan wakibakia wanataabika na machafuko nchini mwao.
“Nimefanya
utafiti wangu hawa wakimbizi wanafunzi wa Sudan wazazi wao ni matajiri wapo
katika nchi za nje wanawasomesha watoto wao wawe mabingwa wa maradhi ya
tropical ili vita itakapomalizika warejee wakafanye kazi nchini mwao,” alisema
Mjengwa.
Amehimiza umuhimu wa kurejea kwenye meza ya maridhiano
kila wakati ambapo nchi inapokuwa kwenye tofauti, na kutahadharisha kuwa nji ya
machafuko huacha madhara makubwa na wakati mwingine hupelekea taifa kutorejea
kwenye amani iliyokuwepo.
Kwa upande wake Mchambuzi wa masuala ya diplomasia
na siasa, Abdulkarim Atik, amewataka vijana nchini kufanya tathmini ya kina
kuhusu ukweli wa taarifa wanazopokea na kusambaza kupitia majukwaa ya
kidijitali. Amesema lengo ni kuepusha taharuki na migawanyiko katika jamii
inayosababishwa na habari za uwongo na propaganda zenye lengo baya.
"Ikiwa vijana watatambua ukweli wa taarifa
wanazopata, itawasaidia kufanya maamuzi sahihi na kuchangia katika kulinda
amani ya nchi hususan kipindi cha uchaguzi," alisisitiza Atik.
Naye Mwandishi wa habari wa Crown Televisheni, Imani
Luvanga, amesisitiza kuwa mitandao ya kidijitali ni nyenzo muhimu ya
mawasiliano na taarifa, na kwamba siyo mibaya kama inavyodhaniwa. Alifafanua
kuwa changamoto kubwa ipo kwa watumiaji, ambao mara nyingi hueneza taarifa
zisizo sahihi na zenye kuchochea migogoro.
Luvanga alieleza kuwa matumizi sahihi ya mitandao ya
kijamii yanaweza kuleta mabadiliko chanya, yakiwemo maendeleo ya kiuchumi.
Alisisitiza umuhimu wa watu kujitambua wanapotumia mitandao hiyo, kwa kuelewa
sababu za kuitumia, aina ya taarifa wanazohitaji, na faida wanazotarajia
kunufaika nazo.
Kwa upande wake, mdau wa siasa na maendeleo, Reeves
Ngalemwa, alisisitiza umuhimu wa kuweka msingi imara wa uzalendo tangu utotoni,
ili kujenga taifa imara.
"Ni muhimu kuweka mazingira ya kuwaandaa watoto
kujifunza uzalendo tangu wakiwa shule za msingi ili wakue wakiwa na mapenzi ya
kweli kwa nchi yao," alisema Ngalemwa.
Aliongeza kuwa lengo la kuanza kuwajenga watoto
katika hatua za awali ni kuandaa kizazi chenye uelewa mpana wa masuala ya
kitaifa, kinachotambua lipi ni sahihi na lipi si sahihi, hususan katika zama
hizi za kidijitali. Ngalemwa alihitimisha kwa kusema kuwa msingi huu imara
utasaidia kujenga Taifa lenye vijana wanaopenda na kulinda maslahi ya nchi yao.
Mchambuzi wa masuala ya vyombo vya habari na mpiga
picha maarufu, Muhidin Michuzi, amesisitiza kwamba wananchi wanatakiwa kujua na
kuyachunguza kwa kina mambo mengi yaliyomo katiukja mitandao kwani mengine ni
propaganda za chuki.
"Watu wanastahili kuangalia kwa umakini sana.
Propaganda inaweza kuwa nzuri au mbaya. Tumefika hapa si kwa bahati mbaya, ni
matokeo ya kuruka hatua. Kila mtu awe mlinzi wa taifa," alieleza Michuzi.
Alionya kuwa kutokuwa na uangalifu katika kusambaza
taarifa hufanya jamii iingie katika migogoro isiyo ya lazima.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TBN , Beda Msimbe
alizungumzia haja ya vijana wa sasa kuwa na ndoto zilizojengwa imara katika
muktadha wa kitaifa na uzalendo huku wakiangalia mambo katika upana wake na si
kuchukua tukio moja tu.
Alisema vijana wanahitaji msingi imara ili maamuzi yao yawe ya kusonga mbele badala ya kuumiza taifa. Lengo ni kuweka maslahi ya Taifa mbele katika matumizi yao ya mitandao ya kijamii na katika kufanya maamuzi ya kisiasa.
Mdahalo huo uliokuwa chini ya Mwenyekiti Jukwaa la Wachambuzi, Magid Mjengwa ulihudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo wahariri wa mawasiliano ya kidijitali, wanabloga kutoka Taasisi ya Tanzania Bloggers Network (TBN), wanafunzi wa Chuo cha Diplomasia, wadau wa amani, na waandishi wa habari.






0 Maoni