'WAANDAMANAJI' WA MTANDAONI: Wasira arejea Kauli ya Rais Samia kuhakikisha Amani

 

Katika kuwahakikishia Watanzania amani na umoja, Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Stephen Wasira, alisisitiza kauli ya utawala kuhusu usalama nchini na kuwataka wananchi wajitokeze kwa wingi kupiga kura bila woga.

Akizungumza mkoani Geita, Wasira alitahadharisha dhidi ya wale wanaoshawishi watu kutokwenda kutopiga kura na kusema: "Hatukubali watu wachache wazuie umma kupiga kura."

Alibainisha kuwa umoja na amani ya nchi ndio msingi wa maendeleo, na akagusa taarifa kuhusu watu wanaojaribu kuzuia zoezi la upigaji kura:

"Nimesikia huko watu wanasema watu wasiende kupiga kura, wako kwenye mitandao wanasema wakati Watanzania wanapiga kura wao wataandamana," alisema Wasira, huku akisisitiza kwamba tarehe ya uchaguzi ni siku ya kupiga kura na "hakuna kuandamana wala mtoto wa maandamano, hamna."

Akithibitisha mamlaka ya serikali, Wasira alirejelea kauli ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyotoa hivi karibuni Dar es Salaam akizungumza viwanja vya Leders katika kampeni za CCM:

"Kama alivyosema Rais (Dk. Samia Suluhu Hassan), juzi, alipokuwa anazungumza Dar es Salaam aliwaambia yeye ndiye Amirijeshi Mkuu, alikuwa hawatishi alikuwa anawaambia tu kwamba kuna serikali ambayo kazi yake ni kuhakikisha amani inakuwepo," alieleza Wasira.

Makamu huyo Mwenyekiti alimalizia kwa kutoa msimamo thabiti wa Chama Tawala, akisema Serikali na CCM "haiwezi kuruhusu uvunjifu wa amani na kuzuia umma wa Watanzania kutumia haki ya kikatiba kuchagua viongozi," na kwamba "Hatuwezi kuruhusu watu wachache wanaotumiwa na watu wa nje kuleta fujo katika nchi yetu."

Alisisitiza kuwa uchaguzi utafanyika kwa amani na kuwataka wapigakura waandamane "kwenda kupiga kura hakuna mtu atawabughudhi hata mmoja, hamna."

Chapisha Maoni

0 Maoni