Tunakwenda Kuboresha Uchumi wa kila MwanaRufiji - Mchengerwa

 

Mgombea wa Ubunge Jimbo la Rufiji Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema endapo wananchi watampa ridhaa ya kumchagua tena katika kipindi atahakikisha kwa pamoja wanafanya ujenzi  wa uchumi kwa  kila mwanarufiji wa jimbo hilo ili kuendelea kuboresha  maisha yao.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kukiombea kura Chama cha Mapinduzi (CCM) kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu kwa ngazi ya Urais, Ubunge na Udiwani katika kata ya Muhoro jimboni Rufiji jana Mhe. Mchengerwa amesema katika  kuhakikisha  miradi mingi ya maendeleo inakwenda kutekelezeka  atakwenda kuiomba serikali  kuweka kituo cha kupozea umeme ili kuwa na umeme  wa uhakika ili  kusaidia kutekeleza miradi mikubwa ya kilimo ambayo tayari wawekezaji wameshajitokeza.

“Tayari tumepata wawekezaji wanaokwenda kujenga viwanda vikubwa  hapa Rufiji, tarafa ya Muhoro, tumeshapata muwekezaji mkubwa ambaye anakwenda kuwekeza  zaidi ya shilingi trioni 1.3 kwenye  kiwanda kikubwa cha ndizi hali ambayo itatufanya  kuuza  ndizi duniani”. Amefafanua Mhe. Mchengerwa.

Amesema  akina mama zaidi ya 1000 na  vijana zaidi ya 6000 wanakwena kujipatia ajira  kwenye  mradi  huu ambapo  amefafanua   kuwa viwanda  vitano  vinakwenda kujengwa  kwenye  tarafa  hiyo ya Muhoro  na kuleta  ajira nyingi  kwa wananchi.

Ametoa  wito kwa  vijana  na wananchi kujiandaa  kimtizamo  na  kuwa tayari kufanya  kazi kwa bidi  ili wawekezaji  hao waweze kuwaajiri  badala  ya kutegemea watu kutoka nje ya maeneo  hayo.

Aidha amewashukuru  kwa  wananchi hao kuendelea  kumchagua  katika vipindi vyote kwa kura  nyingi na kufafanua kuwa wamekuwa wakimchagua  kwa kuwa wamejenga imani kubwa  kuwa ni mtumishi wao ambaye siku zote amekuwa na ndoto za kuwaletea  maendeleo ya kweli.

Leo, Mhe. Mchengerwa anaendelea na mikutano ya hadhara katika kata nyingine za Jimbo hilo kuomba kura kwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa madiwani na kwake mwenyewe ili apewe ridhaa ya kuwaongoza tena katika kipindi hiki.

Mhe. Mchengerwa ni Mbunge wa tisa wa kuchaguliwa katika jimbo hilo la Rufiji toka lianzishwe na kuongozwa na wabunge kadhaa kuanzia mwanasiasa mkongwe nchini hayati  Bibi Titi Mohamed ambapo anaelezewa kuwa ni miongoni mwa wabunge walioliletea maendeleo makubwa Jimbo hilo ukilinganisha na wabunge waliotangulia.

Miongoni  mwa  mafanikio  makubwa  yaliyoletwa  na Mhe. Mchengerwa katika kipindi chake ni pamoja na ongezeko kubwa la Shule za Msingi na Sekondari, zahanati, vituo vya afya na Hospitali, ujenzi wa madaraja, barabara, huduma za maji  na kuvutia wawekezaji katika  jimbo hilo. 


                Na. Yohana Kidaga- Muhoro, Rufiji

Chapisha Maoni

0 Maoni