Mamlaka
ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imeendelea kung’ara kimataifa baada ya
kuthibitishwa kwa mara nyingine kuwa imefanikiwa kushikilia hadhi ya Kiwango
cha Tatu cha Ukomavu (WHO Maturity Level 3) wa mfumo wa udhibiti wa dawa na
chanjo, hatua inayodhihirisha uimara wa mifumo ya afya nchini.
Taarifa
iliyotolewa leo na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA imeeleza kuwa mafanikio hayo
yametokana na tathmini ya kina iliyofanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO)
mwaka 2023, ambayo imethibitisha kuwa TMDA inaendesha shughuli zake kwa uwazi,
weledi na kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vinavyolenga kulinda afya ya
jamii.
“TMDA
inajivunia hatua hii ya mafanikio kwa kuwa inadhihirisha umahiri wa kazi za
udhibiti kwa uwazi, weledi na kwa kufuata viwango vinavyokubalika kimataifa
katika kuhakikisha ubora, usalama na ufanisi wa bidhaa za afya,” imesema sehemu
ya taarifa hiyo.
Mwaka
2018, Tanzania iliweka historia kwa kuwa nchi ya kwanza barani Afrika kupitia
TMDA kufikia kiwango hiki cha tatu cha WHO (ML3), hatua iliyotambuliwa
kimataifa kama kigezo muhimu cha kuaminika katika udhibiti wa dawa na chanjo.
Kuthibitishwa
tena mwaka 2023 baada ya ukaguzi wa kina uliofanywa na WHO ni ushahidi kuwa
TMDA si tu ilifikia viwango hivyo, bali pia imeendeleza mifumo bora ya udhibiti
ambayo ni endelevu na thabiti.
Aidha,
TMDA inasema mafanikio haya yanafungua fursa mpya kwa Tanzania kushiriki kwenye
programu za pamoja za udhibiti wa dawa na vifaa tiba, kuongeza ushiriki kwenye
masoko ya kikanda na kimataifa, na pia kuimarisha mvuto kwa wawekezaji kwenye
sekta ya afya.
TMDA
imewaalika Watanzania wote kusherehekea mafanikio haya kama nchi, na kutoa
shukrani kwa wadau mbalimbali waliotoa mchango wao katika safari hii ya mafanikio.
Kwa
mafanikio haya, Tanzania inaendelea kujijengea hadhi ya kuwa kinara wa mifumo
ya udhibiti wa afya Afrika, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kuhakikisha
ustawi na ulinzi wa afya ya wananchi wake.




0 Maoni