TANAPA kukuza mahusiano ya Kimataifa kupitia Diplomasia ya Utalii

 

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limepokea ugeni kutoka  nchini Italia na kufanya kikao na ili kukuza na kuendeleza mahusiano katika sekta ya uhifadhi na utalii, kikao kilichofanyika  katika Ukumbi wa Mikutano KINAPA.

Kabla ya kikao hicho cha jana, ugeni huo ulipokelewa Octoba 17, 2025 kwa kupanda mlima Kilimanjaro kupitia Lango la Umbwe kwa siku sita na kushuka jana tarehe 22/10/2025 na kushikia lango la Mweka, huku wakijionea vivutio mbalimbali vilivyoko katika mlima huo mrefu kuliko yote duniani kama mlima uliosimama peke yake.

Mbali na shauku yao ya kufika katika kilele cha Uhuru chenye historia ya Taifa letu kwa kupandishwa Bendera ya Taifa na Mwenge wa Uhuru kwa mara ya kwanza Disemba 09, 1961, wageni hao kutoka Italia pia walijikita kutoa elimu ya uhifadhi kupitia kampeni yao iitwayo "SAVE THE MOUNTAINS" ili kuendelea kuhifadhi tunu ya mlima huu.

Akiwakaribisha wageni hao Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi  Maria Kirombo aliwapongeza kwa hatua hiyo inayolenga kuhifadhi Mlima Kilimanjaro kwa manufaa ya Tanzania na dunia kwa ujumla.

Aidha Kamishna Kirombo aliongeza,

"Watalii wanapopanda mlima huu, wengi wao huona mazingira na kutusaidia kutoa maoni yanayotusaidia katika uhifadhi husasani wanaokuja na kampeni kama hii ya “SAVE THE MOUNTAIN AND THEIR CULTURAL HARITAGE” na wengine huungana na jamii inayozunguka hifadhi kwa kupanda miti, sanjari na hilo pia mlima huu ni chanzo cha ajira na kipato kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.”

Naye, Kaimu Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro - Afisa Mhifadhi Mkuu Amri Mtekanga alisisitiza kuwa uhusiano huu usiishie katika zoezi la upandaji wa mlima pekee bali uwe chanzo cha kuibua fursa za uwekezaji na kubadilishana ujuzi wa kiteknolojia unaorahisisha upatikanaji wa mahitaji muhimu hifadhini hususani kwa wapandaji wa mlima pamoja na elimu ya kutosha juu ya tiba na uokoaji pindi dharura inapojitokeza.

Kwa Upande wake Balozi wa Hiari, Bi. Judith Mushi amepongeza serikali ya Tanzania kwa kusaidia mchakato huu kufanikiwa kupitia Ubalozi wa Tanzania nchini Italia kutoa ushirikiano tangu miaka miwili iliyopita alisema, "Nia kubwa ya sisi kuwa hapa ni kufungua milango ya mahusiano na ushirikiano katika uhifadhi na utalii wa milima tukianza na Mlima Kilimanjaro kisha baadae kwenda kwenye maeneo mengine".

Aidha, kiongozi wa msafara huo Bw. Pablo Valoti aliainisha maeneo ambayo Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro inaweza kushirikiana na Chama hicho ili kulinda mazingira yake ni pamoja na kukuza utalii ikiwemo mradi wa uchimbaji maji, mradi wa kudhibiti taka kutoka kwa wageni pamoja na kutoa nafasi za elimu kwa njia ya ufadhili wa masomo ili kwenda kujifunza kwa nadharia na vitendo vile wanachama wanavyofanya katika utunzaji wa milima. 

Sambamba na hilo naye, Ndg. Dario Nisoli alikabidhi barua yenye jumbe anuai ikiwemo ya kuwakaribisha watumishi wa TANAPA kutembelea nchini Italia kujifunza mambo mbalimbali ya uhifadhi na mwendelezo wa sekta ya utalii na kupanua wigo wa ushirikiano baina ya hizo nchi mbili.


                  Na. Calvin Katera - Kilimanjaro

Chapisha Maoni

0 Maoni