Mpina akwama Mahakamani ndoto za kuwania urais 2025

 

Mahakama Kuu Masjala Kuu jijini Dodoma leo imeitupilia mbali kesi iliyofunguliwa na Luhaga Mpina pamoja na chama chake cha ACT-Wazalendo wakipinga kuenguliwa kwake kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.

Katika uamuzi uliotolewa leo Jumatano, Oktoba 15, 2025, mbele ya jopo la majaji watatu, Mahakama hiyo imesisitiza kuwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na sheria zilizopo, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) haiwezi kuingiliwa na chombo chochote kwa maamuzi inayoyafanya ikiwa imeyafanya kwa nia njema na ndani ya mipaka ya kisheria.

Akisoma uamuzi huo, Jaji Fredrick Manyanda ambaye alikuwa kiongozi wa jopo hilo, alisema kuwa hoja zilizowasilishwa na upande wa walalamikaji hazikutosha kuiamuru INEC kubadili uamuzi wake wa kumengua Mpina. Majaji wengine waliokuwa katika jopo hilo ni Sylvester Kainda na Abdallah Gonzi.

Kwa uamuzi huo, Luhaga Mpina hatashiriki rasmi katika kinyang’anyiro cha urais, ambacho tayari vyama mbalimbali vya siasa viko katika harakati za kampeni kuelekea siku ya kupiga kura.

Mpina, aliyekuwa mgombea urais kupitia ACT-Wazalendo, alikuwa amefungua kesi hiyo akiitaka Mahakama Kuu itengue uamuzi wa INEC uliomwengua kwa madai ya kukiuka baadhi ya masharti ya uteuzi.

Chapisha Maoni

0 Maoni