Maelezo Yapongeza Vyombo vya Habari, Yasema Vimetimiza Wajibu Kampeni Zikikaribia Ukingoni

 

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Bw. Rodney Thadeus, ametoa pongezi za dhati kwa vyombo vya habari nchini kwa kutimiza wajibu wao wa kuelimisha umma kwa ufanisi mkubwa tangu kuanza kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu hadi sasa.

Bw. Thadeus aliyasema hayo alipokuwa akihojiwa na mojawapo ya televisheni nchini, akisisitiza kuwa vyombo vya habari vimekuwa nguzo muhimu katika mchakato wa uchaguzi.

"Tumeridhishwa na jinsi vyombo vya habari vilivyochambua habari na kuwalisha wananchi taarifa muhimu kuhusu ilani za vyama, na nini kinastahili kufanyika siku ya kupiga kura,na baadaye " alisema Bw. Rodney.

Alieleza kuwa, mafanikio hayo yamechangiwa sana na vyombo vya habari kufuata Mwongozo kwa Vyombo vya Habari na Waandishi wa Habari katika Kuripoti Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani wa mwaka 2025. Pia, alitaja umuhimu wa mafunzo ambayo yaliendeshwa na Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, yaliyosaidia kuwajengea uwezo waandishi.

Aliongeza kuwa, vyombo vya habari pia vimefanya kazi nzuri ya kuhimiza amani na kuwatanabaisha wananchi umuhimu wa kupiga kura kama haki yao ya kikatiba.

Hata hivyo, Kaimu Mkurugenzi huyo alieleza wasiwasi wake kuhusu baadhi ya vyama vya siasa ambavyo bado havijatoa ilani zao za uchaguzi kwa umma, jambo linaloweza kuwanyima wananchi fursa ya kufanya maamuzi sahihi.

"Ni changamoto kuona kuna vyama bado, mpaka tunapohojiwa, havijatoa ilani zao. Ilani ndiyo dira na ahadi ya chama kwa wananchi," Bw. Rodney alieleza.

Bw. Rodney ametoa wito kwa vyama hivyo kutumia siku chache zilizobaki za kampeni kuelimisha wananchi waziwazi kuhusu nini hasa wanataka kuwafanyia, badala ya kujikita kwenye siasa za kawaida.

"Tunaviomba vitumie siku hizi chache zilizobaki kuelimisha wananchi nini hasa wanataka kuwafanyia. Wananchi wanahitaji kujua mipango ya kina kabla ya kufanya uamuzi wao wa mwisho," alihitimisha.

Kauli hii ya MAELEZO inasisitiza umuhimu wa uwazi na uwajibikaji wa vyama vya siasa katika kuweka bayana ahadi zao kwa wapiga kura, huku ikipongeza jukumu muhimu linalotekelezwa na vyombo vya habari nchini.

Chapisha Maoni

0 Maoni