Madini Chunya kupata nguvu mpya: DC aeleza mikakati kabambe

 

Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mhe. Mbarak Alhaji Batenga, ameweka wazi Mikakati Kabambe ya kuimarisha shughuli za uchimbaji madini Wilayani humo, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa  Kituo cha Umeme (Substation) chenye uwezo wa kuzalisha Megawati 90 hatua inayolenga kupunguza changamoto za upatikanaji wa nishati hiyo kwenye shughuli za madini na nyingine.

Katika mahojiano maalum na timu ya Madini Diary Oktoba 09 2025, Mhe. Batenga alisema kituo hicho kitajengwa katika  eneo la Makongorosi – Chunya  hivyo kitahudumia maeneo ya Chunya na Mkoa wa Songwe, huku akitolea mfano wa Mgodi mpya wa Shanta- New Luika, Mtambo wa uchenjuaji wa  Anglo De Beers  ambao upo mpakani mwa Chunya na Songwe na mgodi mpya wa   Porcupine North  katika  eneo lililoongezwa baada ya upanuzi,  upo Chunya.

Alisema hivi sasa wilaya hiyo inatumia megawati 9 pekee huku mahitaji halisi yakiwa si chini ya megawati 90, na kueleza, ‘’kupitia kituo hiki, tutaanza kuzalisha megawati 45 – lengo ni kufanikisha uchimbaji wa kisasa kwa gharama nafuu, na hivyo kuchochea uwekezaji zaidi. Wachimbaji wetu wanahitaji sana umeme na hapa ninapokea maombi mengi sana ya kufikishiwa nishati hiyo kwenye maeneo yao, na katika hili, nitalisimamia,” alisisitiza Batenga.

 Kutokana na mahitaji hayo makubwa ya umeme hususan kwenye shughuli za uchimbaji, alitoa  wito kwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kutoa  kipaumbele  cha kusambaza umeme kwenye maeneo yenye shughuli za  madini wakati wakipeleka maeneo mengine kutokana na mahitaji makubwa jambo litakalosaidia kupunguza gharama za uzalishaji na hivyo kuongeza uzalishaji na kueleza kwamba,  upatikanaji wa nishati hiyo utasaidia kuvutia  uwekezaji zaidi kutokana na wilaya hiyo kubarikiwa utajiri wa rasilimali  madini na  kugusia ujio wa kampuni ya uchimbaji madini ya  Anglo De Beers ambayo ina baadhi ya leseni zake Chunya huku tayari ikiwa imeanza uchimbaji Songwe  eneo la Mbangala.

Vilevile, alitoa shukrani kwa  Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  kwa kuweka kuipa  kipaumbele  sekta ya madini na hususan wachimbaji wadogo, na kueleza kwamba,  zaidi ya leseni 1,500  zilitolewa kwa ajili ya wachimbaji wadogo  kwa wilaya hiyo na kutoa ombi la kuendelea kutoa leseni zisizoendelezwa ili wale wenye nia ya kuziendeleza wachimbe.

Katika hatua nyingine, aliiomba Wizara ya Madini kufanya tafiti zaidi ili kugundua maeneo mapya yenye madini ili kuwawezesha wachimbaji kuchimba pasipo kubahatisha na kupongeza kwa kutolewa mitambo ya uchorongaji miamba. Kutokana na shughuli za uchorongaji kutokuwa nafuu, alishauri kupatikana mitambo yenye gharama nafuu zaidi ili kuwezesha wachimbaji wadogo kumudu gharama za utafiti, na kusema, ‘’ lakini sisi hatuchimbi tu dhahabu, hivi  sasa  kuna kiwanda cha kuchenjua shaba hivyo ninawaasa wachimbaji waanze kuangalia na madini hayo,’’ alisema.

Katika mazungumzo yake, akayataja  maajabu  ya kipekee  ya  tarafa mbili  zinazounda wilaya hiyo za Kiwanja na Kipambawe, Batenga alisema, “kila moja ni ya kipekee, tarafa ya  Kiwanja ni maalum kwa shughuli za madini na  Kipambawe mahususi kwa kilimo cha tumbaku. Madini hayapo kabisa Kipambawe na hakuna uchimbaji huko na tumbaku haistawi kabisa eneo la  Kiwanja huko kuna kilimo kwa kiasi kidogo tu kwa mazao ya chakula,’’ alieleza.

Akizungumzia mchango wa sekta hizo wilayani humo, alisema hivi sasa Wilaya ya Chunya inachangia asilimia 60 ya fedha za maendeleo kwenye mfuko Mkuu wa Serikali, ikiwa ni ongezeko kubwa kutoka asilimia 40 kwa miaka ya nyuma. “Tunatarajia kuwa ndani ya miaka mitano ijayo, Chunya itachangia hadi asilimia 80, kutokana na mapato ya madini na tumbaku, na kuongeza kuwa hivi sasa Halmashauri, inanufaika kwa kupata kiasi cha shilingi bilioni 5, kutokana na mapato ya sekta hizo mbili kuu, madini na tumbaku.

#Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri

Chapisha Maoni

0 Maoni