Kampuni ya Magellan General Trading LLC yakabidhi gari kwa TAWA

 

Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), imekabidhiwa gari aina ya Toyota Land Cruiser Pick -up na Kampuni ya Magellan General Trading LLC, kwa ajili ya kuimarisha doria za ulinzi wa rasilimali ya wanyamapori katika Hifadhi ya Mkungunero.

Akizungumza wakati wa makabidhiano ya gari hilo yaliyofanyika Oktoba 9,2025, katika Hifadhi ya Mkungunero, Mwakilishi wa Kampuni ya Megallan General Trading LLC, Ahmed Wasama alisema, wao kama wawekezaji mahiri katika Hifadhi ya Mkungunero wametoa gari hilo ili kuendelea kuimarisha shughuli za uhifadhi katika hifadhi hiyo.

Aidha, aliongeza kuwa Megallan itaendelea kushirikiana na TAWA katika masuala yote ya ulinzi, uboreshaji wa miundombinu ya utalii iliyopo katika Hifadhi sambamba na kuendelea kutoa elimu ya uhifadhi kwa vijiji vinavyoizunguka Hifadhi ya Mkungunero.

Kwa upande wake, Kamanda wa Hifadhi ya Mkungunero Floravick Kallambo ambaye alimwakilisha Kaimu Kamishna wa Uhifadhi - TAWA, aliishukuru uongozi wa Kampuni ya Megallan General Trading LLC, kwa kuwapatia gari hilo. Aidha, aliongeza kuwa gari hili litaboresha ufanisi katika shughuli za doria sambamba na kusaidia katika muitikio wa haraka wa matukio mbalimbali ya migongano baina ya wanyamapori na wananchi wanaopakana na hifadhi.

Hifadhi ya Mkungunero inapatikana katika Wilaya ya Kondoa, Mkoa wa Dodoma na imesheheni vivutio mbalimbali ikiwemo mandhari ya kuvutia na wanyamapori mbalimbali kama vile Tembo, Nyati, Twiga, Pofu, Kudu, Choroa na Pundamilia.



Chapisha Maoni

0 Maoni