Dkt. Samia apania kuipaisha Mwanza kiuchumi

 

Mgombea urais wa Tanzania kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameainisha mikakati ya kuinua maendeleo ya Mkoa wa Mwanza akitaja maeneo matatu yatakayochochea uchumi na biashara katika miaka mitano ijayo.

Dkt. Samia ameyasema hayo Jumatano Oktoba 8, 2025 alipohutubia maelfu ya wananchi wa Mkoa wa Mwanza katika mkutano mkubwa wa kampeni uliofanyika Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza.

Ameyataja maeneo hayo kuwa ni ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Mwanza hadi Isaka chenye urefu wa kilometa 314 ambacho ujenzi wake umefikia asilimia 63 na una thamani ya Shilingi trilioni tatu.

Amebainisha kuwa mkoa huo utakuwa na vituo vitano vya kushusha na kupakia abiria na mizigo ambapo vituo hivyo vitachochea shughuli mbalimbali za kiuchumi kama malazi kwa kujengwa mahoteli.Amewahimiza wakazi wa Mwanza kuchangamkia fursa hizo za kiuchumi kwa kuwekeza mkoani humo.

 “Stesheni tano ndani ya Mkoa wa Mwanza ni fursa kubwa ya kiuchumi, ni ajira kwa vijana wetu na kwa watu wa Mwanza kwa ujumla,” amesema Dkt. Samia.

 Mbali ya ujenzi wa mahoteli na maduka katika vituo hivyo, amesema serikali itajenga maghala ya kuhifadhia bidhaa ambazo zitatakiwa kusafirishwa kwenda maeneo mbalimbali ikiwamo Dar es Salaam au nje ya nchi.

Dkt. Samia ameeleza kuwa eneo la Fela kuna bandari kavu ambayo ni fursa nyingine ya kiuchumi na ajira kwa vijana, na kufafanua kuwa reli hiyo itakapokamilika kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza itarahisisha usafiri na usafirishaji pamoja na biashara kwani itatumia muda mchache wa takriban saa nane.

Mgombea huyo amebainisha pia kuwa gharama za usafirishaji na bei zitashuka hivyo itasaidia katika kupunguza mfumuko wa bei na kupunguza kiwango cha umaskini kwani bidhaa zitauzwa kwa bei nafuu.

Dkt. Samia ambaye kwa Mwanza anasema ni nyumbani kwake na anafahamika pia kwa jina la Chifu Hangaya, amelitaja eneo la pili kuwa ni uwekezaji mkubwa uliofanyika katika miradi ya Ziwa Victoria.

Miradi hiyo ni pamoja na ukarabati wa meli ya mizigo ya MV Umoja kwa Shilingi bilioni 19.8 ambayo inafanya kazi na inabeba tani 1,200 za mizigo kwenda Uganda ikifungua masoko mapya kwa wakulima na wafanyabiashara.

“Pia ukiangalia ziwani unaona meli mpya ya kisasa ya MV Mwanza, fahari ya Ziwa Victoria ambayo imewekezwa zaidi ya Shilingi bilioni 120 na sasa imekamilika kwa asilimia 98 na wiki mbili zilizopita ilifanya majaribio ndani ya ziwa na wanamalizia asilimia mbili ili meli ianze safari zake,” alieleza Dkt. Samia aliyefanya mikutano minne mikubwa katika mkoa huo kitovu cha biashara na uchumi Kanda ya Ziwa.

Amesema meli hiyo itakuwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo na gari 20 pamoja na malori makubwa matatu yanayovuka kwenda nchi nyingine kwa wakati mmoja, akisema “hiyo sio meli tu, bali ni alama ya heshima na uwezo wetu wa kujiletea maendeleo kwa fedha zetu wenyewe”.

Ametaja pia upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini kwa gharama ya Shilingi bilioni 18.6,ukarabati na ujenzi wa vivuko vipya vitano vitakavyochochea shughuli za kiuchumi, na pia kupeleka boti za doria, na za kubeba wagonjwa katika Kisiwa cha Ukerewe.

Kwa upande wa Kiwanja cha Ndege cha Mwanza amesema kinaenda kukamilika na kuwa cha kimataifa ili kurahisisha njia ya watalii kwenda Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na hivyo kukuza sekta ya utalii.

Kwenye kilimo, Dkt. Samia amewapa faraja wakulima wa pamba kwa kusema serikali imesambaza mbegu na dawa bure na imeajiri maofisa ugani 700 kwa kushirikiana na sekta binafsi kukuza zao hilo.

Aidha, amesema tayari matrekta 700 yameagizwa na 350 yameshawasili nchini na yatagawiwa kwa wakulima ambayo watayakodi kwa nusu bei, na yatawekwa katika vituo vya zana za kilimo katika kanda.

Kwenye viwanda, ametaja hatua za kufufua viwanda vya kusafisha pamba pamoja na Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza na kukijengea uwezo ili kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwamo zinazotumika hospitalini.

Ametangaza neema katika matumizi ya maji nchini akisema mbali ya kutumika kwa wananchi yakiwamo kutoka Ziwa Victoria, baada ya kukamilika kwa Gridi ya Taifa ya Maji, kinachofuata ni kuyatumia maji hayo kwa umwagiliaji ili yalipe fedha zinazotumika sasa kupeleka maji ya kunywa kwa wananchi.

“Kwa hiyo tumeamua maji kutoka katika maziwa yetu tutayatumia katika kujenga Gridi ya Maji Kitaifa na kuyatumia kwa kilimo cha umwagiliaji ili njiani yanapopita wananchi wa Tanzania wayatumie kwa kumwagilia mashamba na tupate mavuno makubwa zaidi,” alieleza.

Amesema wanafanya hivyo kwa sababu serikali ya CCM ina ajenda ya kukuza sekta ya kilimo ambayo kwa sasa inakua kwa asilimia tano lakini lengo ni kuifanya sekta hiyo ifikapo mwaka 2030 ikue kwa asilimia 10.

Katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro amempokea mwanachama mpya wa CCM kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambaye alikuwa ni Katibu wa Mkoa wa Mwanza, Boniface Mkobe aliyesema amehama kwa sababu Chadema imekuwa ikihamasisha vurugu na chuki na kufarakanisha wananchi.

Na. Aboubakary Liongo - Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM

Chapisha Maoni

0 Maoni