Mgombea
wa nafasi ya Rais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye pia ni
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali
Mwinyi, amesema Serikali itaendelea kujenga masoko katika kila wilaya na mkoa
ili kuandaa mazingira bora zaidi kwa wajasiriamali nchini.
Akizungumza na makundi mbalimbali ya Wajasiriamali,
waendesha bodaboda na bajaji, Wajane, Wavuvi na Wakulima katika mkutano wa
hadhara wa kampeni uliofanyika katika
Uwanja wa Michezo wa Kihinani, Mkoa wa Mjini Magharibi leo tarehe 18 Oktoba
2025, Dkt. Mwinyi amesema hatua hiyo inalenga kuwawezesha wajasiriamali kufanya
biashara katika mazingira salama, ya kisasa, na yenye tija.
Halikadhalika,
Dkt.Mwinyi ameeleza kuwa Serikali itaendelea kuwapatia wajasiriamali mafunzo ya
biashara na alama za ubora ili bidhaa zao ziweze kufikia viwango vya kimataifa
na kuhimili ushindani wa soko la kikanda na kimataifa.
Kuhusu
tozo za masoko, Dkt. Mwinyi amesema Serikali italifanyia kazi suala hilo kwa
lengo la kuhakikisha wajasiriamali wanatozwa viwango rafiki vinavyorahisisha
shughuli zao za kila siku. Aidha, aliahidi kujenga vituo vya mabasi vyenye
maeneo maalum kwa bodaboda, na kutoa mikopo nafuu kwa wajasiriamali baada ya
kurasimisha biashara zao.
Katika
sekta ya kilimo, Dkt. Mwinyi amebainisha kuwa Serikali itaendelea kuimarisha
skimu za umwagiliaji, kuwapatia wakulima pembejeo, mbolea za bei nafuu, na mafunzo
kupitia mabwana shamba ili kuongeza uzalishaji na kujitosheleza kwa chakula.
Kwa
upande wa uvuvi, amesema Serikali itaendeleza ujenzi wa masoko ya kisasa na
madiko, pamoja na viwanda vya kusarifu samaki katika eneo la Fungu Refu kwa
lengo la kuongeza thamani ya mazao ya baharini, sambamba na ujenzi wa gati
jipya katika eneo la Kihinani.
Akizungumzia
masuala ya kijamii, Dkt. Mwinyi amesema Serikali itaweka adhabu kali kwa wazazi
wanaotelekeza watoto wao ili kukomesha tabia hiyo, na ameahidi kuwawezesha
wajane kupitia mikopo isiyo na riba na mafunzo ya kujikwamua kiuchumi.
Amesisitiza
kuwa Serikali itaendelea kuweka utaratibu mzuri wa uendeshaji wa masoko ili
yawe safi, rafiki kwa wajasiriamali, na kulinda haiba ya miji ya Zanzibar.
Vilevile,
Dkt. Mwinyi ametangaza kuwa tarehe 29 Oktoba 2025, siku ya kupiga kura, itakuwa
siku ya mapumziko, na amewataka wananchi wote kujitokeza kwa wingi kushiriki
katika Uchaguzi Mkuu huo.
Kabla ya
kuanza kuhutubia wananchi, Dkt. Mwinyi alipiga simu kwa Katibu Mkuu wa Wizara
ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Bi. Fatma Hamad Rajab, aliyekuwa
katika Uwanja wa New Amaan Complex ambako timu za KMKM na Azam FC zilikuwa
zikicheza mechi ya raundi ya michuano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika.
Kupitia salamu hizo, aliwatakia mchezo mwema na kuwakumbusha wanamichezo pamoja
na wananchi wote umuhimu wa kujitokeza kupiga kura.
Akiwahitimishia
wananchi wa Kihinani, Dkt. Mwinyi ameomba kupewa tena ridhaa ya kuiongoza
Zanzibar kwa awamu nyengine, akiahidi kuendeleza juhudi za kuleta maendeleo
makubwa zaidi kwa wananchi wote wa Zanzibar.



0 Maoni