CCM yaahidi kuendelea kuimarisha kinga ya jamii kupitia wahudumu wa afya ngazi ya jamii

 

Chama Cha Mapinduzi CCM kimeahidi kuendelea kuimarisha huduma za kinga ndani ya jamii kupitia program kabambe ya Wahudumu wa Afya ngazi ya jamii ambao wamewezeshwa kwa mafunzo na kupewa vifaa kwa ajili ya kutoa huduma za msingi za afya pamoja na elimu ya afya ndani ya jamii.

Akitumia zaidi ya dakika 30 akiwa amepiga magoti kunadi sera za CCM na kuomba wananchi kukipigia kura za ndio CCM kupitia wagombea wake, Mgombea Ubunge katika Jimbo la Peramiho, Jenista Mhagama akiwa katika Kata ya Kizuka katika Wilaya ya Songea Vijijini amesema Mgombea wa nafasi ya Urais Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anayo nia njema ya kuimarisha huduma za kinga kupitia wahudumu hao wa afya ngazi ya jamii.

“Mgombea wa urais wetu pamoja na kuongeza ajira za watumishi wa afya, kupitia Serikali tayari alishaanzisha kundi la wahudumu maalum wanaojulikana kama wahudumu wa afya ngazi ya jamii, na hapa tayari wameshachukuliwa na kupata mafunzo na kazi yao kubwa ni kupita nyumba kwa nyumba kutoa huduma za afya kwa haraka,” amesema Mhagama.

Amesema kuwa wahudumu wanamchango mkubwa katika kuimarisha huduma za kinga ndani ya jamii ambapo pia husaidia katika kutambua na kushiriki katika jitihada za udhibiti dhidi ya magonjwa ya mlipuko hatarishi yanayoweza kuleta athari kwa wananchi.

“Wahudumu hawa ni watoto wetu, wataendelea kuhudumiwa na Serikali ya CCM, watalipwa posho na Serikali, na huyu ndiyo jabali mbobezi Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesema Mhagama.

Mhagama amewaomba wananchi ifikapo Otoba 29, 2025 kwenda kukipigia kura za ndio CCM kupitia wagombea wake kuanzia mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yeye mwenyewe anayeombea nafasi ya Ubunge pamoja na Madiwani wanaogombea kupitia CCM ili waendelee kuwaletea maendeleo wananchi.

Kupitia Programu hii iliyozinduliwa mwaka 2024, kiasi cha zaidi ya Shilingi Bilioni 899 kimepangwa kutumika ndani ya miaka mitano kwa ajili ya mafunzo ya darasani na vitendo, ununuzi wa vitendea kazi pamoja na kulipa posho za wahudumu zaidi ya 137,294 ambao wataajiliwa katika mikoa yote 26 ya Tanzania Bara.



Chapisha Maoni

0 Maoni