Naibu
Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu,
Zuhura Yunus, amewataka wakulima wadogo na wasindikaji wa zao la zabibu kuwa
mabalozi wa mabadiliko chanya ili kukuza ujuzi wa kuongeza thamani ya mazao
kwenye mnyororo wa mazao ya kilimo.
Zuhura
Yunus ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya kuongeza ujuzi kwa wakulima na
wasindikaji wadogo katika sekta ya kilimo leo (21 Oktoba, 2025) jijini Dodoma,
yanayolenga kuongeza weledi na ujuzi kwa wakulima wapatao 1,000 nchini.
“Lengo
kuu la mafunzo haya ni kuongeza ufanisi katika uzalishaji, kuimarisha njia za
utendaji kazi ili kuongeza ubora wa bidhaa na kutoa huduma bora zaidi katika
sekta ya kilimo,” alisema Naibu Katibu Mkuu Zuhura Yunus.
Aidha,
amesema wakulima na wazalishaji wadogo huchangia katika uzalishaji wa mazao ya
chakula nchini na kutoa malighafi kwa viwanda, lakini wamekuwa na changamoto ya
upungufu wa ujuzi wa mnyororo wa thamani, ndiyo maana Ofisi ya Waziri Mkuu –
Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu imeandaa mafunzo hayo kwa kushirikiana na
Wizara ya Kilimo.
Wakizungumza
kwa niaba ya washiriki, Bi. Mary Uguzi ameishukuru Serikali kwa kuendelea
kuwapatia ujuzi wenye tija. Naye Noha Madeje amesema kuwa kupitia mafunzo
waliyopata wamejifunza vitu vingi katika utengenezaji bora wa mvinyo. Hata
hivyo, wanufaika hao wameiomba Serikali kuendelea kuwapatia mikopo
itakayowawezesha kukuza biashara zao.
Kwa
upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI),
Dkt. Thomas Bwana, ambaye anaongoza timu ya wataalam kufundisha wakulima hao,
aliwashauri kuwa watumie elimu na ujuzi watakaoupata kwenda kuwafundisha wenzao
ili tija inayokusudiwa iweze kupatikana.
Dkt.
Bwana aliongeza kusema kuwa TARI imejipanga kuhakikisha matokeo ya tafiti
wanazozifanya yanawafikia na kuwasaidia wakulima na wasindikaji wa bidhaa za
kilimo nchini ili tija ipatikane na kuchangia ukuaji wa uchumi.
Naye
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ajira na Ukuzaji Ujuzi, Alana Nchimbi, alieleza
kuwa mafunzo haya baada ya kufunguliwa leo, yatatolewa katika mikoa minne na
aina ya mazao yatakayohusika kwenye mafunzo hayo ni: Dodoma – Zabibu,Singida –
Alizeti, Iringa – Nyanya na mchicha lishe na Mbeya – Maharage na parachichi, ambapo
jumla ya wakulima 250 kwenye kila mkoa watanufaika.
Alana
aliongeza kuwa Ofisi hiyo inaratibu mafunzo hayo kwa kushirikiana na wadau ili
kuwezesha nguvu kazi katika sekta mbalimbali kupata ujuzi stahiki kupitia
Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi (Up-skilling Training) kwa mwaka wa fedha
2025/2026.

0 Maoni