Shirika
la Kimataifa la African Wildlife Foundation (AWF) imeikabidhi rasmi Mamlaka ya
Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) majengo maalum kwa ajili ya Kikosi cha
Mbwa Nusa (TAWA K9-UNIT) kwa lengo la kuimarisha ulinzi wa rasilimali ya
wanyamapori katika maeneo ya Mipakani mwa Nchi, Vituo vya Ushuru wa Forodha na
Viwanja vya Ndege vya Kilimanjaro na Arusha.
Akizungumza
jana katika hafla ya uzinduzi na makabidhiano ya jengo la Kikosi cha Mbwa Nusa
zilizofanyika katika Ofisi za TAWA, Kanda ya Kaskazini zilizopo jijini Arusha,
Mgeni Rasmi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAWA, Mej.Jen
(Mstaafu) Hamis Semfuko amesema Kikosi cha mbwa nusa (Sniffing dogs) ni nyenzo
muhimu ambayo imekuwa ni msaada katika kudhibiti uhalifu unaohusiana na
usafirishaji haramu wa nyara za Serikali na biashara haramu ya wanyamapori.
“Kikosi
hiki kimekuwa msaada mkubwa hasa katika kudhibiti utoroshaji nyara kupitia
mipakani, vituo vya usafirishaji na forodha,” amesema Semfuko.
Mej.Jen
(Mstaafu) Semfuko ameongeza kuwa TAWA itaendelea kukiimarisha Kikosi hiki kwa
kuongeza idadi ya watumishi katika kikosi, kuongeza vitendea kazi pamoja na
kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa watumishi wa kikosi cha Mbwa Nusa.
Sambamba
na hilo, Mej.Jen (Mstaafu) Semfuko amewashukuru AWF kwa mchango wao uliowezesha
ujenzi wa jengo la (TAWA-K9 UNIT). Aidha, ametoa rai kwa wadau wengine wa
Uhifadhi kuendelea kushirikana na TAWA katika kuimarisha ulinzi wa rasilimali
ya wanyamapori.
Kwa
upande wake, Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la AWF, Pastory Magingi, amesema Jengo
hili limekabidhiwa kwa ajili ya kuimarisha utekelezaji wa sheria kupitia mbwa
waliopatiwa mafunzo, sambamba na kuwapatia mbwa hawa makazi ya kudumu.
Pamoja na
hilo, Bw. Magingi ameongeza kuwa AWF kwa kushirikiana na TAWA imeweza kuandaa
miongozo mbalimbali kwa ajili ya uendeshaji wa vikosi vya mbwa wa uhifadhi.
Awali,
akitoa salamu za ukaribisho, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA, Mlage Yussuf
Kabange amesema mashirikiano mazuri yaliyopo baina ya TAWA na AWF yameweza
kufanikisha ujenzi wa jengo hilo ambalo linajumuisha vyumba sita (6) vya mbwa,
Ofisi, Stoo ya chakula, maliwato na eneo la wazi lenye uzio kwa ajili ya
mazoezi ya mbwa.
Vilevile,
Kamishna Kabange ameongeza kuwa pamoja na Mbwa Nusa (Sniffing dogs), TAWA
imepanga kuanzisha Kikosi cha Mbwa wa ufuatiliaji (Tracking dogs) na kuanzisha
Kituo cha mafunzo ya Mbwa (Dog Training Centre).
Naye,
Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi TAWA, Segoline Tarimo ambaye alimwakilisha
Kamanda wa Kanda ya Kaskazini amesema tangu kuanzishwa kwa Kikosi cha Mbwa,
Kikosi kimepata mafanikio mengi ikiwemo kudhibiti uhalifu wa utoroshaji wa
nyara kupitia kiwanja cha KIA na maeneo ya mipakani.
Kadhalika,
ameongeza kuwa majengo haya yaliyokabidhiwa yatawezesha kikosi kufanya kazi
katika mazingira bora na kwa ufanisi zaidi.
Hafla hii
ya makabidhiano ya Jengo la Kikosi cha Mbwa Nusa, iliambatana na kusaini
makubaliano (Memorandum of Understanding) baina ya AWF na TAWA. Makubaliano hayo yalijikita katika matumizi
ya Mbwa Nusa na matumizi ya teknolojia katika kudhibiti uhalifu wa
nyara za wanyamapori.
Na. Joyce
Ndunguru - Arusha



0 Maoni