13 Wasaka rekodi Mlima Kilimanjaro wapanda wakiwa wameziba midomo

 

Kundi la watalii waliojipambanua kupanda na kushuka mlima Kilimanjaro kwa masaa 24 wakitokea katika mataifa mbalimbali barani Ulaya, kama “Inspire Challenge Group” lilianza safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro siku mbili (2) zilizopita na kufanikiwa kufika kilele na kushuka kwa muda huo kupitia lango la Marangu, huku washiriki wake wakipumua kwa kutumia pua pekee baada ya kuziba midomo yao.

Hii inakuwa ni “challenge” ya kwanza na ya kipekee ya kuweka rekodi mpya ndani ya Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro (KINAPA). Kama ilivyo kawaida watu wengi wanapopanda milima wakati mwingi hutumia njia mbili katika upumuaji hasa unapokuwa unahema kwa sababu ya kutembea kwa haraka au unapopanda sehemu iliyoinuka.

Safari hiyo ya kipekee imeanzia katika Hoteli ya Selig mjini Moshi ambako washiriki hao walifanya mazoezi mepesi, yakiwemo yale yanayolenga kuimarisha upumuaji kwa kutumia pua pekee.

Baada ya maandalizi hayo, kundi hilo lilielekea langoni Marangu, ambako walipokea maelekezo ya usalama, kufanya usajili rasmi, na kugawiwa viziba midomo kabla ya kuanza kupanda mlima kuelekea Kilele cha Uhuru, ambacho ni sehemu ya juu kabisa barani Afrika yenye urefu wa mita 5895 kutoka usawa wa bahari.

Safari hiyo pia imekuwa kivutio kwa wadau wa utalii, wakiwemo viongozi wa KINAPA na mashirika ya utalii, wanaoamini kuwa “challenge” hiyo itachochea utalii wa ustahimilivu na kuongeza hamasa kwa watalii wengi kuja na “challenge” nyingine tofauti ndani ya Mlima Kilimanjaro.

Safari hiyo ya kuvutia na yenye mvuto wa aina ya kipekee imeratibiwa na kampuni ya utalii ya Thomas Safaris & Treks Limited, ikihusisha jumla ya washiriki 13 kutoka nchi za Italia, Ufaransa, Uswisi na Ubelgiji, huku ikishirikisha timu ya wasaidizi 30 wakiwemo waongoza watalii, wapishi na wabeba mizigo.

  Na. Jacob Kasiri - Kilimanjaro

Chapisha Maoni

0 Maoni