UN yaitaja Tanzania kinara ongezeko la watalii Afrika

 

Tanzania imetajwa kuwa nchi inayoongoza barani Afrika kwa ongezeko la watalii, kwa mujibu wa Shirika la Utalii Duniani la Umoja wa Mataifa (UN World Tourism Organization). Taifa hili limepata kutambuliwa kwa kuwa na ongezeko kubwa zaidi la idadi ya watalii baada ya janga la UVIKO-19, likifikia kiwango cha ukuaji cha asilimia 48.

Hayo yameelezwa wakati wa maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani, ambayo hufanyika kila mwaka tarehe 27 Septemba. Kwa mwaka huu, kilele cha maadhimisho hayo kilifanyika katika Eneo la Hifadhi la Ngorongoro (picnic site).

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, alisema kuwa kiwango cha ukuaji wa Tanzania kilikuwa kikubwa zaidi kuliko cha Ethiopia (asilimia 40), Morocco (35%), Kenya (11%) na Tunisia (9%).

Aidha, alieleza kuwa ripoti ya utalii ya mwaka 2025 kutoka UN Tourism imeitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi 20 bora duniani zinazofanya vizuri zaidi katika sekta ya utalii, kwa wastani wa ukuaji wa zaidi ya asilimia 50.

Kati ya mwaka 2021 hadi 2024, idadi ya watalii wa kimataifa iliongezeka kutoka 922,692 hadi 2,141,895, sawa na ongezeko la asilimia 132.1. Utalii wa ndani pia uliongezeka kwa kasi kubwa kutoka 788,933 hadi 3,218,352, ongezeko la asilimia 307.9.

Ifikapo Desemba 2024, jumla ya watalii wa ndani na wa kimataifa ilikuwa 5,360,247, ongezeko la asilimia 107.2.

Mapato yatokanayo na utalii yaliongezeka kutoka dola bilioni 1.3 za Marekani mwaka 2021 hadi dola bilioni 3.9 mwaka 2024, ikiwa ni ongezeko la asilimia 200.

Dkt. Abbasi alisema mafanikio haya yametokana na jitihada za Serikali katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020–2025, ambayo inalenga kufikia watalii milioni 5 na mapato ya dola bilioni 6 za Marekani ifikapo mwaka ujao.

Kuanzia Januari hadi Julai 2025, idadi ya watalii iliendelea kuongezeka kwa asilimia 9.2, ikifikia milioni 1.27, ikilinganishwa na milioni 1.16 katika kipindi kama hicho mwaka 2024.

Aliisifu Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuboresha miundombinu, kutumia teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), pamoja na kuitangaza Tanzania kupitia filamu kama “The Royal Tour” na “Amazing Tanzania”, ambazo zimechangia kuiweka nchi katika ramani ya dunia ya utalii.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kauli mbiu:

“Utalii na Mabadiliko Endelevu” (Tourism and Sustainable Transformation), ikilenga kuhamasisha ubunifu, taaluma, maendeleo ya biashara na ushirikishwaji wa jamii katika ukuaji wa utalii.





Chapisha Maoni

0 Maoni