Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia
Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Almas Kisabya, ameahidi kutoa
mashine za kielektroniki za ukusanyaji mapato (EFD) bure kwa wafanyabiashara
wote nchini, ikiwa atachaguliwa kuongoza serikali.
Kisabya alitoa kauli hiyo jana, Jumapili Septemba 7, 2025,
wakati wa uzinduzi rasmi wa kampeni za chama hicho uliofanyika katika eneo la
Soko la Matunda, Kata ya Chem Chem, Manispaa ya Tabora.
“Ndani ya siku 30 tu baada ya kuunda Baraza la Mawaziri,
kipaumbele chetu kitakuwa kuhakikisha EFD zinatolewa bure kwa wafanyabiashara
kote nchini. Hili ni jukumu la serikali, si mzigo wa mwananchi,” alisema
Kisabya.
Aidha, mgombea huyo alieleza kuwa chama chake kinapanga
kuhusisha mashirika ya umma kama Tanesco katika mfumo wa ukusanyaji wa mapato,
akisema taasisi hiyo imeonesha mafanikio makubwa katika udhibiti wa makusanyo
bila kuathiri mahusiano yake na wateja.
“Ikiwezekana, Tanesco tutawatumia kusaidia katika ukusanyaji
wa mapato, maana wameweza kufanikisha makusanyo yao bila migogoro na wananchi,”
alisisitiza.
Katika hatua nyingine, Kisabya aliahidi kuhakikisha wananchi
wanapata huduma ya maji bure, kwa kutumia mitambo ya nishati jadidifu kama sola
na upepo katika kusambaza maji vijijini na mijini.
“Utaalamu upo, teknolojia ipo. Tukitumia mfumo huu, gharama
za upatikanaji wa maji zitashuka kwa kiasi kikubwa. Tunataka kuhakikisha kila
Mtanzania anapata maji safi bila kikwazo,” alisema.
Kampeni za NRA zimezinduliwa kwa kaulimbiu ya "Tanzania Mpya, Maisha Bora Kwa Wote", huku mgombea huyo akiahidi kuwa chama chake kitatoa kipaumbele kwa miradi ya kijamii inayogusa maisha ya wananchi wa kawaida.
0 Maoni