Mgombea
urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha Wakulima (AAFP),
Kunje Ngombale Mwiru, amesema kuwa endapo atapata ridhaa ya kuongoza nchi
katika Uchaguzi Mkuu wa 2025, hatapenda kuona Mtanzania yeyote anaendelea
kuishi kwenye nyumba ya nyasi.
Mwiru alitoa
kauli hiyo Septemba 2, 2025, katika mkutano wa kampeni uliofanyika kata ya
Matombo, Jimbo la Morogoro Kusini, akitokea kata ya Kisaki, ambako alikuwa
akihutubia wananchi na kuelezea vipaumbele vyake iwapo atachaguliwa kuwa Rais.
“Ndugu
zangu, maendeleo hayahitaji hasira wala jazba. Kwa kipindi changu cha miaka
mitano, sitapenda kuona Mtanzania yeyote anaishi kwenye nyumba za nyasi, iwe ni
mwana-Matombo au wa sehemu nyingine yoyote nchini,” alisema Mwiru.
Alisema kuwa
Tanzania ina viwanda vya kutosha vya kuzalisha mabati, hivyo kupitia
ushirikiano na viongozi wa wilaya na mikoa, ataweka utaratibu wa kubaini idadi
ya wananchi wanaoishi kwenye nyumba za nyasi ili kuhakikisha wanajengewa nyumba
zenye mabati.
Miundombinu, mawasiliano na ajira kwa
vijana
Mbali na
makazi bora, Mwiru alisema serikali yake itahakikisha kila kaya inapata huduma
ya mawasiliano ya simu ili kuwawezesha wananchi kuwasiliana moja kwa moja na
viongozi wao wa ngazi ya wilaya na mkoa.
“Serikali
yangu itakuwa ya mchakamchaka, ya saa 24. Itafanya kazi bila kupumzika. Hii
itaongeza ajira kwa vijana. Sio kwamba ajira hakuna, bali mazingira ya vijana
kupata ajira ndio hayajatengenezwa,” alisisitiza.
Mwiru
alieleza kuwa ana mpango wa kuanzisha viwanda vya kuchakata vyakula, matunda na
hata kuchonga mawe maeneo ya vijijini ili kutoa ajira kwa vijana bila
kulazimika kwenda Dar es Salaam.
“Ile dhana
ya kwamba mtu lazima aende Dar es Salaam kutafuta kazi viwandani si ya kweli.
Hata huku kwetu kuna sifa za kuanzisha viwanda. Tutatengeneza mazingira bora ya
uwekezaji vijijini,” aliongeza.
Walimu na wastaafu kupewa kipaumbele
Katika
hotuba yake, Mwiru aliweka msisitizo maalum kwa walimu, akisema kuwa serikali
yake itawajengea nyumba bora, kuboresha mazingira yao ya kazi na kuongeza
mishahara yao kwa kutambua mchango wao katika jamii.
“Mwalimu
ndiye anayemfundisha Profesa, hata fisadi. Kwa hiyo, mwalimu anapaswa kupewa
heshima kubwa, si kuishi kwenye nyumba za buibui bila umeme. Serikali yangu
haitavumilia hali hiyo,” alisema.
Aidha,
alisema wastaafu wenye afya njema wataendelea kushiriki katika kazi za
kuimarisha taifa kupitia mafundisho ya uzalendo na maadili, huku akiweka mpango
wa kuanzisha madarasa maalum ya kuwahusisha katika kutoa elimu hiyo kwa vizazi
vijavyo.
“Tutawawezesha
wastaafu wanaoweza kufanya kazi waendelee kufundisha uzalendo na maadili. Huu
ndio msingi wa Taifa imara,” alisema.
Awataka wakulima kutokubali
kudanganywa
Akihitimisha
hotuba yake, Mwiru aliwataka wakulima kujitambua na kutokubali kudanganywa na
wanasiasa wa vyama vingine, akisisitiza kuwa AAFP ni chama chao halisi.
“Msidanganywe
kwamba kuna mwanasiasa wa chama kingine atakayekuja kuwasemea wakulima. Kama
mkitutosa AAFP, mmewatosa wakulima wenzenu. Chagueni chama chenu, mchagueni
mkulima mwenzenu,” alihitimisha.
0 Maoni