Tembo 500 kuhamishwa Kitengule kwenda Hifadhi ya Burigi-Chato

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa kushirikiana na wadau wengine wa Uhifadhi mkoani Kagera limeanza rasmi operesheni ya kuwahamisha Tembo zaidi ya 500 waliokuwa kwenye Bonde la Kitengule, na kuwapeleka Hifadhi ya Taifa Burigi–Chato. Hatua hiyo inalenga kulinda maisha ya wananchi, mali zao, pamoja na  mashamba ya wakulima na wawekezaji kutokana na uharibifu uliokuwa ukisababishwa na wanyama hao.

Zoezi hilo limezinduliwa jana tarehe 2 Septemba 2025 na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mhe. Hajat Fatma Mwassa, katika viwanja vya Kiwanda cha Sukari Kagera. Amewahakikishia wananchi kwamba changamoto na madhara yaliyokuwa yakisababishwa na Tembo kuvamia makazi na mashamba sasa yanakwenda kufika kikomo.

"Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amefanya kazi kubwa ya kuhakikisha wanyama hawa aina ya Tembo wanahamishwa kurudishwa kwenye Hifadhi ya Taifa Burigi-Chato, aidha ametuma wataalam na helikopta ili kuwahamisha Tembo zaidi 500 waliopo katika Bonde la Kitengule," alisisitiza Mkuu wa Mkoa Mhe. Mwassa.

Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Dkt. Fredrick Mofulu, amewahakikishia wananchi usalama katika zoezi zima la kuwahamisha Tembo hao.

Wakati huo huo, mwekezaji wa Kiwanda cha Sukari Kagera alibainisha kuwa kwa muda mrefu Tembo wamekuwa wakiathiri mashamba ya miwa na kusababisha upotevu mkubwa wa mazao. Alisema utekelezaji wa zoezi hili utasaidia kuokoa zaidi ya tani 200,000 za miwa kwa mwaka zenye thamani ya shilingi za Tanzania bilioni 6.


                       Na. Hance Mbena - Kagera


Chapisha Maoni

0 Maoni