Mtandao
wa Wanablogu Tanzania (TBN) umepiga hatua kubwa katika safari yake ya
kuhalalishwa kitaaluma baada ya kukabidhiwa rasmi hati za uanachama wa Baraza
la Habari Tanzania (MCT), katika Mkutano Mkuu wa 27 wa Baraza hilo uliofanyika
Septemba 25, 2025, jijini Dar es Salaam.
TBN ni
miongoni mwa wanachama wapya wanane waliojiunga na Baraza hilo, hatua
inayotajwa kuwa ya kihistoria katika kuimarisha sauti na nafasi ya wanablogu
katika tasnia ya habari nchini.
Akizungumza
mara baada ya hafla ya makabidhiano, Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, alisema
uanachama huo ni zaidi ya heshima ni chombo cha ulinzi na utetezi wa haki za wanablogu.
"Uanachama
huu unatoa uhalali na kutambuliwa rasmi kwa wanablogu mbele ya jamii, Serikali
na wadau wengine. Tunajumuishwa katika familia kubwa ya vyombo vya habari
vinavyojisimamia, na sasa wanablogu wanatambulika kama chanzo cha habari
kinachowajibika," alisema Msimbe.
Msimbe
alibainisha kuwa kupitia MCT, wanablogu sasa wana fursa ya kunufaika na mfumo
wa usuluhishi wa Baraza, hususan katika kushughulikia malalamiko yanayoweza
kujitokeza kutokana na kazi zao.
"Mfumo
huu unawalinda wanablogu kisheria na kiuchumi dhidi ya vitisho au kufilisiwa
kutokana na faini za kimahakama, kwa kuwa sasa wana kimbilio katika Kamati ya
Maadili ya MCT," aliongeza.
MCT Yasisitiza Mshikamano wa Wanachama
Katibu
Mtendaji wa MCT, Ernest Sungura, alisisitiza kuwa mafanikio ya Baraza
yanatokana moja kwa moja na uimara wa wanachama wake.
"Kauli
mbiu ya mwaka huu inasema ‘Uhai wa Wanachama ni Nguvu na Usalama wa Taaluma ya
Habari’. Ikumbukwe ni wanachama waliokubaliana kwamba tujisimamie au tukubali
kufa," alisema Sungura.
Alionya
kuwa enzi za kutegemea wafadhili zimeshaisha, na sasa Baraza linategemea
wanachama wake kwa uhai na maendeleo yake.
Makamu
Mwenyekiti wa Bodi ya MCT, Yusuf Khamis Yusuf, alisisitiza kuwa kwa miaka 30
tangu kuanzishwa kwa Baraza hilo mwaka 1995, limejipambanua kama nguzo ya
maadili na weledi nchini.
"Kusimama na Haki ni Sadaka" – Jaji Mihayo
Mkutano
huo ulifunguliwa rasmi na Jaji Mstaafu Thomas Mihayo, Rais Mstaafu wa Nne wa
Baraza, ambaye aliwakumbusha wanahabari kuhusu dhamana waliyo nayo mbele ya
jamii.
"Kusimama
kwenye haki ni kugumu kuliko kujipendekeza. Kusimama na haki kunahitaji sadaka.
Siyo njia nyepesi au rahisi, lakini ni njia ya baraka mno na ni njia
inayompendeza Mungu," alisisitiza Jaji Mihayo.
Alieleza
kuwa uwepo wa MCT umeokoa vyombo vingi vya habari dhidi ya kufilisiwa, na kwamba
ni jukumu la kila chombo wakiwemo wanablogu kuwa kiungo cha ukweli bila kuegemea upande
wowote.
Katika
hatua nyingine muhimu, Jaji Mihayo alizindua rasmi Tuzo za Umahiri wa Uandishi
wa Habari Tanzania (EJAT 2025), ambazo mwaka huu zitaendeshwa kwa mfumo wa
kidijitali sambamba na uzinduzi wa tovuti mpya ya MCT hatua inayoashiria
dhamira ya Baraza katika kukuza weledi na teknolojia kwenye tasnia ya habari.



0 Maoni