Shangwe!
Furaha! Nderemo na Vifijo vilirindima katika kijiji cha Kalalani baada ya
Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) chini ya Mwenyekiti wake wa Bodi
ya Wadhamini - Mkuu wa Majeshi (Mstaafu) Jenerali George Waitara alipokabidhi
Kituo kipya cha Polisi - Kalalani ili kuimarisha ulinzi wa wananchi na mali
zao.
Ujenzi wa
Kituo hicho uligharimu kiasi cha shilingi takribani milioni 150.62 ikihusisha
jengo lenye vyumba zaidi ya 8, eneo la mapokezi, mifumo ya maji safi na maji
taka pamoja na mifumo ya umeme ikiwa ni utamaduni wa TANAPA kurudisha faida ya
uhifadhi na utalii kwa jamii zinazozunguka Hifadhi za Taifa nchini ili
washiriki katika ulinzi wa maliasili.
Hata
hivyo, Kituo cha Polisi Kalalani kitakuwa ni mwarobani wa kero zote za
kiusalama ambazo wananchi hao walikuwa wakizifuata umbali wa zaidi ya kilometa
30 hususani katika kijiji cha Masewa.
Akikabidhi
mradi huo kwa Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Kamishna wa Uhifadhi (Mstaafu) Mhe.
William Mwakilema kwa niaba ya wananchi hao, Jen. Waitara alisema;
“Ujenzi
wa kituo hiki ni muhimu sana ukizingatia kijiji hiki cha Kalalani kiko mpakani
mwa nchi, hivyo matarajio ya ulinzi na usalama ni mkubwa, hivyo niwaase
wanakijiji wa Kalalani na vijiji vya jirani kufanya kazi kwa ukaribu na Jeshi
la Polisi watakaotumia kituo hiki.”
Akikata
utepe wakati wa makabidhiano ya kituo hicho kuashiria kufunguliwa kwake, Mhe.
Mwakilema alisema, “Niwasisitize wananchi wa Kata ya Kalalani, jengo hili licha
ya sababu za kiusalama pia ni pamoja na kuimarisha ulinzi wa hifadhi yetu ya
Mkomazi.”
Kwa
upande wake, Kamishna Msaidizi wa Polisi Joseph Ng’weve akimwakilisha Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Tanga aliwashukuru TANAPA kwa msaada huo alisema kuwa kituo
hicho kitakuwa mkombozi kwa wananchi wa Kalalani na maeneo ya jirani ambayo kwa
muda mrefu yalikosa huduma ya karibu ya ulinzi wa polisi.
Naye,
Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji cha Kalalani Orolonyo Tulakani alisema kuwa
wamepokea mradi huo kwa furaha na matumaini makubwa kwani utasaidia kupunguza
matukio ya uhalifu na kuongeza amani.
Makabidhiano
hayo yanaashiria ushirikiano na mshikamano kati ya majeshi haya mawili katika
kusimamia ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao kwa ajili ya maendeleo
endelevu.
Hafla ya
uzinduzi wa Kituo hicho cha Polisi Kalalani ilifanyika leo Septemba 22, 2025
Katika kijiji cha Kalalani katika Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga ambapo
wanakijiji hao walitoa Ekari 3 za ardhi
kwa ajili ya ujenzi wa Mradi huo.
Na. Jacob
Kasiri - Tanga.
0 Maoni