Dkt. Samia Aahidi Kujenga Chuo cha Uhasibu Ruvuma

 

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameahidi kujenga Kampasi ya Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) katika mkoa wa Ruvuma, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha elimu ya juu nchini.

Dkt. Samia ametoa ahadi hiyo leo wakati akijinadi mbele ya maelfu ya wananchi waliojitokeza katika mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye viwanja vya Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) mjini Songea, mkoani Ruvuma.

Amesema kuwa hatua hiyo inalenga kuongeza fursa za elimu ya juu kwa vijana wa mkoa huo na kanda nzima ya kusini, pamoja na kuandaa wataalamu wa masuala ya fedha, biashara na usimamizi wa rasilimali kwa kiwango cha kitaifa na kimataifa.

“Kampasi hii ya Chuo cha Uhasibu Arusha itakapokamilika, itakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi zaidi ya 10,000 kwa wakati mmoja. Nawaambia wana Ruvuma: jiandaeni kuwa wahasibu wa baadaye,” alisema Rais Samia huku akishangiliwa na umati wa watu.

Rais Samia, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, amesema serikali ya chama hicho itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya elimu na kuongeza vyuo vikuu na vya kati katika maeneo mbalimbali nchini, ili kuhakikisha elimu inawafikia wananchi wote bila ubaguzi wa kijiografia.




Chapisha Maoni

0 Maoni