TAKUKURU Tanga yaokoa milioni 10.5 kwenye mradi wa barabara

 

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Tanga imefanikiwa kuokoa kiasi cha shilingi milioni 10.5 baada ya kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi wa barabara ya kiwango cha lami katika Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, ikiwa ni sehemu ya miradi ya maendeleo ya sekta ya barabara.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Tanga, Mkuu wa TAKUKURU mkoa huo, Ramadhani Ndwatah, alisema kuwa fedha hizo ziliokolewa baada ya kubainika kuwepo kwa upungufu wa nguzo tatu za taa za umeme wa jua kwenye barabara yenye urefu wa mita 830, ambayo ilipaswa kuwa na nguzo 29 lakini ziliwekwa 26 tu.

“Huu ni mfano halisi wa namna taasisi yetu inavyotekeleza wajibu wa kuhakikisha fedha za umma zinatumika ipasavyo,” alieleza Ndwatah na kuongeza kuwa hatua stahiki zilichukuliwa mara moja kwa kuwasiliana na TARURA (W) ili kuhakikisha kasoro hizo zinatekelezwa kwa haraka.

Ndwatah aliongeza kuwa hatua hiyo ilisaidia kurejeshwa kwa nguzo hizo tatu zenye thamani ya Shilingi milioni 10.5, zilizowekwa kwa viwango stahiki kulingana na mkataba na BOQ ya mradi husika. Alisisitiza kuwa hilo ni jukumu muhimu la TAKUKURU katika kuzuia upotevu wa rasilimali za taifa.

Aidha, katika kipindi cha Aprili hadi Juni 2025, TAKUKURU Tanga ilifuatilia miradi 29 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 7.9, ambapo miradi 10 kati ya hiyo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 2.8 ilibainika kuwa na changamoto mbalimbali za kiutekelezaji.

“Baadhi ya miradi haikulipiwa VAT, mingine haikufuata michoro rasmi au kucheleweshwa kinyume cha mikataba,” alisema Ndwatah huku akibainisha kuwa mamlaka husika zimejulishwa kwa hatua za kiutawala na kisheria kuchukuliwa.

Kwa mujibu wa Ndwatah, TAKUKURU itaendelea kufuatilia kwa karibu matumizi ya fedha katika miradi ya maendeleo, huku pia ikitilia mkazo elimu kwa umma kuelekea uchaguzi mkuu wa 2025.


Chapisha Maoni

0 Maoni