RC Makalla aipongeza TANAPA kwa kusimamia vyema uhifadhi na utalii

 

Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Makalla leo Septemba 21, 2025 ametembelea na kufanya Kikao Kazi na Menejimenti ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) katika Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara iliyopo Mto wa Mbu mkoani Arusha.

Katika kikao chake na Menejimenti ya TANAPA Mhe. Makalla alipokea taarifa ya jumla ya Shirika kutoka kwa Kamishna wa Uhifadhi - TANAPA pamoja na kufanyiwa mawasilisho ya utendaji kazi kutoka kwa Wakuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha na Ziwa Manyara ambazo zipo mkoani Arusha na kuipongeza TANAPA kwa kuendelea kusimamia vema shughuli za Uhifadhi na Utalii katika maeneo yote ya Hifadhi za Taifa hapa nchini.

"Niwapongeze sana kwa kusimamia maeneo haya ya Uhifadhi. TANAPA mna dhamana kubwa ya kuendeleza Uhifadhi na Utalii wa nchi yetu kwa kuvilinda na kuviendeleza vivutio na rasilimali tulizojaaliwa na Mwenyezi Mungu katika nchi yetu. Niwahakikishie mtapata ushirikiano mkubwa kutoka kwangu.

"Hifadhi za Taifa ni maeneo yaliyotengwa kisheria na mipaka yake inajulikana. Kuharibika kwa maeneo haya mliyokasimiwa kuyasimamia kwa niaba ya watanzania ni jambo ambalo halipaswi kutokea kwani mara nyingi kunasababishwa na watu wengine wasio na mapenzi mema kutanguliza ubinafsi mbele. Hakikisheni mnafanya kila jitihada kuendeleza Uhifadhi kwani Utalii ni matokeo ya Uhifadhi. Mtalii atakuja kuona nini kama hujahifadhi?" alisema Mhe. Makalla.

Naye, Kamishna wa Uhifadhi TANAPA  CPA Musa Nassoro Kuji alibainisha kuwa TANAPA imejidhatiti vilivyo katika kulinda na kuendeleza rasilimali zote zilizopo katika Hifadhi za Taifa na kuongeza kuwa  TANAPA itaendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa.

Aidha, Kamishna Kuji aliongeza kuwa katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, TANAPA imeshuhudia idadi kubwa ya wageni katika maeneo yote yanayosimamiwa na Shirika.

Pongezi zetu zimfikie Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani kupitia filamu ya "Tanzania: The Royal Tour" na ile ya "Amazing Tanzania" zimeleta mapinduzi makubwa katika sekta ya utalii nchini ambapo kwa hali ilivyo sasa ni vigumu kutofautisha kati ya "High season" na "Low season" kwani tunashuhudia idadi kubwa ya watalii katika  vivutio vyetu".

Mhe. CPA Amos Makalla yupo kwenye ziara ya kikazi katika taasisi na maeneo mbalimbali mkoani Arusha ikiwa ni sehemu ya kukutana na wadau pamoja na kuwatia moyo watumishi na wananchi ili kila mmoja ajione kuwa anayo nafasi katika kuchangia uchumi wa Mkoa wa Arusha na Taifa kwa ujumla.


            Na. Edmund Salaho - Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara

Chapisha Maoni

0 Maoni