Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limetangaza kuanza kwa kampeni
maalum ya usalimishaji wa silaha haramu kwa hiari, kampeni itakayodumu kwa
kipindi cha miezi miwili kuanzia Septemba 1 hadi Oktoba 31, 2025.
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari, Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Mbeya, SACP Benjamin Kuzaga, amesema kampeni hiyo inalenga kuwawezesha
wananchi wanaomiliki silaha kinyume cha sheria, kwa kujua au kutokujua,
kuzisalimisha bila kuchukuliwa hatua za kisheria.
“Mwananchi yeyote anayemiliki silaha haramu anatakiwa
kusalimisha silaha hiyo kwa hiari katika ofisi za Serikali za Mtaa au Kijiji
kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa 10:00 jioni, au katika kituo chochote cha
Polisi kilicho karibu naye,” alisema SACP Kuzaga.
Ameeleza kuwa kwa watakaojitokeza ndani ya muda huo maalum,
Jeshi la Polisi halitachukua hatua yoyote ya kisheria, lakini baada ya
kumalizika kwa kampeni hiyo, operesheni kali itafanyika kwa lengo la kuwabaini
na kuwachukulia hatua wote watakaokaidi agizo hilo.
“Baada ya Oktoba 31, 2025, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya
litaanza operesheni maalum na msako mkali dhidi ya wale wote watakaobainika
kuendelea kumiliki silaha kinyume cha sheria,” alionya Kamanda huyo.
SACP Kuzaga ametoa rai kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa
Jeshi la Polisi kwa kuhakikisha wanawajulisha wengine kuhusu tangazo hilo, ili
kuondoa kisingizio cha kutokufahamu taarifa hiyo pindi muda wa kampeni
utakapoisha.
Aidha, amewahimiza wananchi kuwa wazalendo kwa kushiriki kikamilifu katika kampeni hiyo kwa ajili ya kulinda amani na usalama wa jamii.

0 Maoni