Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia
Chama cha ACT-Wazalendo, Luhaga Mpina, ametangazwa rasmi kuwania nafasi hiyo na
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), siku chache kupita baada ya Mahakama Kuu
kumrejesha kwenye kinyang’anyiro hicho.
Mpina aliteuliwa rasmi baada ya kuwasilisha fomu zake kwa
Mwenyekiti wa INEC, Jaji mstaafu Jacobs Mwambegele, katika ofisi ndogo za tume
hiyo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza baada ya zoezi hilo, Jaji Mwambegele alisema
Tume imeamua kuwapatia wagombea wote wa urais gari moja kila mmoja, pamoja na
dereva, kwa ajili ya kusaidia kampeni zao.
“Tume imeamua kumpatia kila mgombea gari moja pamoja na
dereva kwa matumizi ya kampeni, ili kuweka usawa,” alisema Jaji Mwambegele.
Hata hivyo, Chama cha ACT-Wazalendo kimekataa kupokea gari
hilo aina ya Toyota Land Cruiser GX VXR lililotolewa na Tume kwa ajili ya
kampeni.
Mwanasheria Mkuu wa chama hicho, Omar Shaban, alisimama na
kueleza kuwa chama hakitahitaji kutumia rasilimali hiyo.
“Kwanza tunashukuru sana kwa ukarimu mliotuonyesha, lakini
tumependelea kutochukua gari. Tupo vizuri na tunaomba rasilimali hiyo isaidie
kwenye matumizi mengine,” alisema Shaban.
Akijibu uamuzi huo, Jaji Mwambegele alisema tume haina
shinikizo kwa chama chochote kupokea gari hilo, akieleza kuwa lengo lilikuwa ni
kuhakikisha usawa katika kipindi cha kampeni.
“Sawa, ni mapenzi yenu. Lengo la magari haya lilikuwa ni
kuweka usawa katika kampeni, lakini kama hamtalihitaji, tume italitumia kwa
matumizi mengine,” alisema.
Hatua hiyo ya uteuzi wa Mpina inafuatia uamuzi wa Mahakama Kuu wiki hii, uliomrejesha rasmi kwenye mchakato wa uchaguzi baada ya kushinda kesi aliyofungua dhidi ya INEC, akipinga kuenguliwa kwake katika mchakato wa awali wa uteuzi.
0 Maoni