Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kupitia Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Wilson Elias Mulumbe,
amesema serikali ya ADC itahakikisha kila halmashauri nchini inakuwa na magari
ya kisasa ya kuchimba visima ili kuondoa kabisa tatizo la maji safi na salama
kwa wananchi.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni
uliofanyika leo katika Kata ya Kingolwira, Mtaa wa Bomba la Zambia mkoani
Morogoro, Mulumbe amesema tatizo la maji limeendelea kuwa kero kwa wananchi
wengi, hasa vijijini, na ni muda sasa hatua madhubuti zichukuliwe kulimaliza.
“Tunataka wananchi wetu waache kuteseka kwa
kukosa huduma ya msingi kama maji. Serikali ya ADC itahakikisha kila
halmashauri inapata gari la kuchimba visima ili kila mtu apate maji safi na
salama,” alisema Mulumbe.
Mbali na sekta ya maji, mgombea huyo ameahidi
kuboresha huduma nyingine muhimu za kijamii zikiwemo elimu, afya, nishati na
miundombinu ya barabara, akieleza kuwa huduma hizo zitapewa kipaumbele katika
mipango ya maendeleo ya ADC.
Katika hatua nyingine, Mulumbe alisema
serikali yake itaweka wenyeviti wa serikali za mitaa kote nchini kwenye mfumo
rasmi wa malipo kwa kuwalipa mishahara, ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wao
mkubwa katika kusimamia maendeleo ya wananchi.
“Wenyeviti wa mitaa ni wawakilishi wa wananchi
wa ngazi ya chini kabisa. Tunataka nao watambulike rasmi kwa kazi zao kwa
kupewa stahiki kama watumishi wengine wa umma,” alisema.
Mulumbe alisisitiza kuwa chama cha ADC kina
dira na mikakati madhubuti ya kuleta maendeleo ya kweli kwa Watanzania wote,
kwa kusimamia kwa ufanisi rasilimali za taifa, kuimarisha uwazi katika utawala
na kupambana na ubadhirifu wa mali za umma.
Kampeni za uchaguzi mkuu zinaendelea kushika kasi huku wagombea mbalimbali wakiendelea kuwasilisha sera na ahadi zao kwa wananchi. Uchaguzi mkuu unatarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
0 Maoni