Kiwanda cha kusafisha Graphite Godmwanga, tafsiri ya Tanzania ya viwanda

  

Wakati dunia ikipiga hatua kuelekea kupunguza matumizi ya nishati inayozalisha hewa ukaa na kuongeza matumizi ya nishati safi, viwanda vya kusafisha madini ya kinywe (graphite) vya Godmwanga Gems vinaibuka kuwa tafsiri ya ujenzi wa Tanzania ya viwanda na jinsi madini yanavyochochea ukuaji wa viwanda Tanzania.

Viwanda hivyo viwili vinavyopatikana katika Vijiji vya Kwedikabu na Kwamsisi Wilayani Handeni Mkoa wa Tanga,  vinamilikiwa na Mtanzania Godlisten Mwanga, kwa asilimia 100 na kutumia rasilimali za madini za Tanzania, kwa kuchakata na kugeuza kinywe ghafi kuwa tayari kwa matumizi ya viwandani.

Viwanda hivyo ni vya kwanza nchini Tanzania kuanza uzalishaji wa madini Kinywe na kuifanya Tanzania kuwa nchi ya tatu barani Afrika baada ya Madagascar na Msumbiji na kuhakikishia nafasi ya Tanzania kama kiungo muhimu katika usambazaji wa bidhaa hiyo muhimu duniani.

Septemba 08, 2025, Akizungumza na Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Madini, Meneja wa Kiwanda B, Henry Joseph alieleza kuwa, kuanzishwa kwa viwanda hivyo kumesaidia kuimarisha nafasi ya Tanzania katika uchumi wa kijani (green economy) kutengeneza ajira kwa wenyeji, utengenezaji na ukarabati wa miundombinu ya afya, elimu, barabara, ukuaji wa kiuchumi sambamba na kuonesha jinsi madini yanavyoweza kuwa nguzo muhimu ya ukuaji wa viwanda nchini.

Uwekezaji wa Viwandani na Teknolojia

Viwanda vya Godmwanga vina uwezo wa kuchakata na kusafisha graphite hadi kiwango cha juu cha asilimia 95 kinachokubalika kimataifa. Hatua inayofanya Tanzania kuwa msambazaji wa malighafi muhimu kwa sekta kama betri za umeme, vifaa vya kiteknolojia na vilainishi vya viwandani, mashine muhimu na magari hivyo kuwa sababu ya kuanzishwa kwa viwanda vingine vinavyotegemea malighafi hizi.

Ajira, Mafunzo, na Uwezo wa Jamii

Kupitia mafunzo ya kazi, mafunzo ya ufundi, na mpangilio wa usalama kazini, wakazi wa Kata ya Kwamsisi na vijiji vya jirani wanapata ajira za moja kwa moja viwandani na ajira zisizo za moja kwa moja kupitia mnyororo wa thamani (supply chain). Hii inaongeza mapato ya kaya, kuboresha elimu na kuongeza mahitaji ya huduma za afya na biashara ndogo ndogo. Uwezo huu wa kibinafsi ulipelekea kuundwa kwa wajasiriamali wadogo waliokuwa wazalishaji wa vipuri, huduma za usafiri, uchumi na maendeleo endelevu kwa wakazi.

 Ushindani wa Kimataifa na Fedha ya Kigeni

Kwa kutoa graphite yenye ubora wa juu, Kampuni Godmwanga imefanikiwa kuingia katika masoko ya nje, hususani Marekani, China na Korea Kusini huku ikileta fedha za kigeni. Mapato haya pia yanasaidia Serikali kuwasilisha Sera za kuendeleza sekta ya madini kwa njia endelevu.

Uendelevu na Ushirikiano wa Jamii

Viwanda vimetengeneza ajira rasmi zaidi ya 616 wengi wakiwa ni wakazi wa maeneo ya jirani na miradi hiyo. Kampuni ya Godmwanga pia inashirikiana na jamii kupitia Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR) kwa kutengeneza na kukarabati  miradi ya kijamii kama shule, vituo vya afya na miundombinu ya barabara.

Jinsi Viwanda Vinavyobadili Maisha ya Wakazi wa Kwamsisi

Subira Hasssan na Hellen David ni miongoni mwa wafanyakazi wa Kiwanda cha Godmwanga Gems Ltd, wanakiri kuwa uwepo wa mradi huo umesaidia kuyabadili maisha yao binafsi pamoja na vijiji vya Kwedikabu, Kwamsisi na maeneo ya jirani kwa kuleta ajira rasmi na zisizo za moja kwa moja. Miradi hii na mengine katika Wilaya ya Handeni, taratibu imeondoa simulizi maarufu za Kwamsisi na kuleta taswira mpya ya maendeleo.

Mwanzo wa Taifa Lenye Viwanda Vinavyosimamiwa na Rasilimali

Simulizi ya Godmwanga ni mfano wa jinsi Kampuni moja inaweza kuwa kivutio cha mabadiliko: kutoka mgodi mdogo hadi mfululizo wa viwanda vinavyochangia ukuaji wa taifa. Kwa kuingiza teknolojia, kuwekeza kwa wananchi, na kushirikiana na Serikali na jamii, madini siyo tu rasilimali ya kuuza bali vyanzo vya kuendeleza viwanda, kuimarisha uchumi, na kubadilisha mustakabali wa kizazi kipya.

Kwa mujibu wa Utafiti wa Shirika la Nishati la Kimataifa (International Energy Agency- IEA) uliofanyika Mei 2025, unaonesha kuwa mahitaji ya jumla ya Kinywe mnamo 2024 yalikuwa tani milioni 4.8, mahitaji ya sekta ya teknolojia safi pekee yalifikia tani milioni 1.5. IEA inakadiria mahitaji ya jumla kufikia tani milioni 8.219 ifikapo mwaka 2030 .

Madini ya Kinywe hutumika kutengeneza betri za magari, magari ya umeme, vilainishi vya mitambo muhimu, vituo vya utafiti kwa teknolojia ya nishati, vifaa vya utafiti wa anga na viwanda vya kutengeneza vifaa vya elektroni na kadhalika.

Godmwanga Gems Ltd inaonesha jinsi madini  pale yanapochakatwa kwa ubunifu na kuyaongezea thamani yanavyoweza kuwa kiini cha kuzalisha viwanda, kutengeneza ajira, kuvutia uwekezaji, na kuendeleza miundombinu ya Taifa. Ni mfano wa wazi wa azma ya Tanzania ya viwanda vinavyotokana na rasilimali zake zikiwemo za madini kama Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025-2050 inayoelekeza.

Chapisha Maoni

0 Maoni