INEC yatoa angalizo kwa Chama cha ACT Wazalendo kuhusu Luhaga Mpina

 

Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) imekitaka Chama cha ACT Wazalendo kuzingatia masharti ya Kanuni ya 35 ya Kanuni za Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani za mwaka 2025, inayohusu utaratibu na ratiba za ubunge, ili kuhakikisha mchakato wa uchaguzi unaendeshwa kwa mujibu wa sheria na miongozo iliyowekwa.

Kauli hiyo ya INEC imekuja kufuatia taarifa iliyochapishwa kwenye tovuti rasmi ya ACT Wazalendo tarehe 21 Septemba 2025, ikieleza kuwa kutakuwa na uzinduzi wa Ilani ya Uchaguzi wa chama hicho katika Makao Makuu ya chama, tukio litakalofuatiwa na uzinduzi wa kampeni za ubunge katika Jimbo la Segerea.

Taarifa hiyo ya chama pia ilieleza kuwa shughuli hizo mbili zitahudhuriwa na waliotajwa kuwa ni wagombea wa kiti cha Rais na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia ACT Wazalendo, ambao ni Ndugu Luhanga Joelson Mpina na Ndugu Fatma Abdulhabib Ferej.

Hata hivyo, INEC kupitia taarifa rasmi iliyotolewa na Mkurugenzi wa Uchaguzi, Kailima Ramadhani Kailima, imeweka wazi kuwa kwa mujibu wa uamuzi wake wa tarehe 15 Septemba 2025, ACT Wazalendo haina mgombea wa kiti cha Rais wala Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, baada ya kutengua rasmi uteuzi wa Ndugu Luhanga Joelson Mpina.

Chapisha Maoni

0 Maoni