Chama cha
Ukombozi wa Umma (CHAUMMA) kimeahidi kushughulikia tofauti kubwa za mazingira
ya kazi kwa watumishi wa umma nchini endapo kitapewa ridhaa ya kuongoza
Serikali katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.
Ahadi
hiyo imetolewa jana na mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia
chama hicho, Salum Mwalimu, wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika katika
Kata ya Majimoto, Wilaya ya Mpimbwe, mkoani Katavi.
Akihutubia
mamia ya wananchi waliojitokeza kumsikiliza, Mwalimu amesema kuwa moja ya
kipaumbele cha Serikali atakayoiongoza ni kuhakikisha kuwa watumishi wa umma
wanalipwa mshahara wa chini usiopungua Sh 800,000 kwa mwezi, baada ya makato,
ili kuwawezesha kuishi kwa heshima na kujikimu katika mazingira yoyote
wanayofanyia kazi.
“Tunataka
mtumishi wa umma popote alipo mjini au kijijini ajisikie thamani ya utumishi
wake. Haiwezekani mtumishi wa kijijini mwenye changamoto nyingi apokee mshahara
sawa na yule wa mjini pasipo kuzingatia mazingira yao ya kazi,” alisema
Mwalimu.
Amesisitiza
kuwa watumishi wengi wa umma wanaohamishiwa maeneo ya pembezoni hukumbwa na
hali ngumu ya maisha, huku wengine wakihisi kama wameadhibiwa, jambo ambalo
amesema litakomeshwa mara moja iwapo CHAUMMA kitashinda.
“Tunataka
kujenga mfumo wa ajira wa haki na wa kutia moyo. Mtumishi wa umma anatakiwa
afurahie kulitumikia taifa, si kuhisi kama ameachwa au kutelekezwa kwa sababu
ya mahali alipopelekwa,” aliongeza.
Katika
hotuba yake, Salum Mwalimu pia aliwataka watumishi wa umma na wananchi kwa
ujumla kuendelea kuwa na matumaini, akisisitiza kuwa CHAUMMA inatambua
changamoto nyingi zinazoikabili sekta ya utumishi wa umma, hasa maeneo ya
vijijini, na kwamba chama hicho kina sera mahususi za kuzitatua kwa njia ya
kudumu.
Ahadi
hiyo imepokelewa kwa hisia mseto kutoka kwa wananchi waliokuwa uwanjani, ambapo
baadhi yao wameeleza matumaini kwamba sera hizo zikitekelezwa zinaweza
kubadilisha hali ya maisha ya watumishi wengi walioko maeneo ya mbali.
CHAUMMA
ni miongoni mwa vyama vinavyoshiriki uchaguzi mkuu wa mwaka huu kwa mara ya
tatu tangu kimesajiliwa rasmi mwaka 2015, na kimekuwa kikisisitiza ajenda za
usawa wa kijamii, haki katika ajira na maboresho ya maslahi ya wafanyakazi.
0 Maoni