EU yatoa tahadhari kuhusu kupungua kwa barafu Mlima Kilimanjaro

 

Umoja wa Ulaya (EU) umetahadharisha kuhusu kasi ya kupungua kwa barafu katika Mlima Kilimanjaro, hatua inayotajwa kuathiri kwa kiasi kikubwa mazingira na maisha ya jamii zinazotegemea rasilimali za mlima huo.

Akizungumza jana Septemba 19, 2025 wakati wa ziara ya Waheshimiwa mabalozi wa Umoja wa Ulaya waliotembelea Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro, Balozi wa Finland Nchini Tanzania. Mhe. Theresa Zitting amesema hali ya kuyeyuka kwa barafu katika kilele cha Uhuru ni ishara ya wazi ya mabadiliko ya tabianchi yanayoikumba dunia.

“Ni jambo la kusikitisha kusikia na kushuhudia jinsi barafu inavyopungua na namna hali hiyo inavyotarajiwa kuathiri mtiririko wa maji na mfumo wa ikolojia katika maeneo ya chini ya mlima. Tatizo hili halipo Tanzania pekee; hata nchini mwangu Finland tunashuhudia mabadiliko ya joto,” alisema.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, takribani watalii 60,000 hutembelea  Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro kila mwaka, wengi wao ni kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya.

Hata hivyo, viongozi hao wameelezea hofu ya kupungua kwa barafu na mabadiliko ya tabianchi kunaweza kudhoofisha kivutio hicho cha kimataifa endapo hatua madhubuti hazitachukuliwa.

Katika mikakati yake ya kimazingira, EU kupitia balozi wake hapa nchini Bi. Christine Grau alisema wamejipanga kuendeleza ushirikiano na Tanzania kupitia sera za Green Deal zinazolenga kufikia usawa wa sifuri wa kaboni na kutimiza malengo ya Mkataba wa Paris.

Pia, EU  imesisitiza dhamira yake ya kuisaidia Afrika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi bila kuibebesha mzigo wa uchafuzi wa mazingira uliosababishwa na bara la Ulaya.

Aidha, Umoja wa Ulaya umesisitiza umuhimu wa kulinda misitu ya Tanzania, ikiwemo kuongeza misitu ya kupandwa na kudhibiti ukataji hovyo ili kudumisha mfumo wa ikolojia unaochangia kupunguza hewa  ya ukaa.

Kwa sasa, takribani asilimia 55 ya eneo lote la Tanzania limefunikwa na misitu, hali ambayo wataalamu wanasema ni ngao muhimu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi.

EU imeahidi kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika uhifadhi endelevu wa misitu, maendeleo ya kilimo rafiki kwa mazingira, na kubadilishana teknolojia za kukabiliana na changamoto za tabianchi.

“Tunachokiona hapa ni mfano wa changamoto za kidunia zinazohitaji mshikamano wa kidunia. Mlima Kilimanjaro ni urithi wa dunia, na jukumu la kuutunza ni letu sote,” alihitimisha Balozi huyo wa EU.

Afisa Uhifadhi Mwandamizi ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Utalii KINAPA, Stephen Moshy, alisema ziara hiyo imewapa nafasi ya kueleza fursa zilizopo katika hifadhi na jinsi jamii zinazozunguka mlima huo zinavyonufaika na rasilimali zake.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro, Amri Mtekanga, alisema mabalozi hao walipata nafasi ya kujifunza kuhusu shughuli mbalimbali za utalii, ikolojia na usimamizi wa mazingira katika hifadhi hiyo unaofanywa na TANAPA.

Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro (KINAPA) imepokea ugeni wa mabalozi wa Umoja wa Ulaya kutoka nchi 12, hatua inayotajwa kuwa fursa kubwa kwa utalii na ushirikiano wa kimataifa na utachagiza ongezeko la watalii katika hifadhi hiyo siku za usoni.




Chapisha Maoni

0 Maoni