Doyo aibua kero tano za Geita atakazozitatua

 

Mgombea urais wa Chama cha National Liberation for Democracy (NLD), Doyo Hassan Doyo, ameibua kero tano zinazowakabili wananchi wa Mkoa wa Geita, huku akiahidi kuzitatua endapo atachaguliwa kuwa Rais katika Uchaguzi Mkuu..

Akihutubia wananchi katika mikutano ya kampeni iliyofanyika jana Septemba 29, 2025 katika eneo la Stendi ya Zamani, Jimbo la Sengerema, na baadaye Kata ya Buseresere, Doyo alisema changamoto hizo zimekuwa ni kilio cha muda mrefu kwa wananchi wa Geita na maeneo mengine ya Kanda ya Ziwa.

Katika hotuba yake, Doyo alitaja kero kubwa kuwa ni ubovu wa barabara unaosababisha gharama kubwa za usafiri kwa wananchi, hali inayochangia ugumu wa maisha na kudidimiza shughuli za kiuchumi.

“Barabara mbovu ni adui wa maendeleo. Zinawafanya wananchi walipie gharama kubwa kufikisha bidhaa sokoni, wagonjwa kushindwa kufika hospitali kwa wakati, na hata wanafunzi kuchelewa mashuleni. Tutashughulikia hili ndani ya mwaka wa kwanza,” alisema.

Kero ya pili aliyoitaja ni ukosefu wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya afya vya umma, akieleza kuwa hali hiyo inahatarisha maisha ya wananchi, hasa wa kipato cha chini.

“Ni jambo la kusikitisha kuona mama mjamzito anakwenda kliniki anakosa hata vidonge vya kuongeza damu. Serikali inapaswa kuwekeza kwenye afya ya watu wake,” aliongeza.

Doyo pia aliibua changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama, akisema kuwa bado kuna vijiji na kata nyingi ndani ya Geita ambavyo havina huduma ya uhakika ya maji, hali inayowaathiri zaidi wanawake na watoto.

Kero nyingine ni kukosekana kwa masoko yenye tija kwa wakulima, ambapo alisema kuwa mazao mengi ya wakulima yanaharibika au kuuzwa kwa hasara kutokana na ukosefu wa miundombinu bora na sera rafiki za masoko.

“Wakulima wameachwa bila dira. Tutaanzisha mifumo ya uhakika ya masoko, kuongeza thamani ya mazao na kuhakikisha mkulima anafaidika na jasho lake,” aliahidi.

Doyo alihitimisha kwa kueleza kuwa endapo wananchi watamchagua, atahakikisha mikakati iliyopo ndani ya Ilani ya NLD inatekelezwa kwa vitendo, huku akiahidi kuanza kushughulikia kero hizo tano ndani ya mwaka mmoja wa kwanza madarakani.

Chapisha Maoni

0 Maoni