Dkt. Samia: CCM ni chama kinachotimiza ahadi zake

 

MGOMBEA urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema tofauti ya chama hicho na vyama vingine ni kuwa CCM inapoahidi inatekeleza huku ikijua itatekeleza vipi na wapi itapata fedha za utekelezaji.

Dkt. Samia ameyasema hayo jana Septemba 22, 2025 kwenye Viwanja vya VETA Msamala wilayani Songea mkoani Ruvuma alipohutubia maelfu ya wananchi waliojitokeza kusikiliza Ilani ya chama hicho katika mkutano wa kampeni za Uchaguzi Mkuu.

Akiwa na mgombea mwenza Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, Dkt. Samia amesema wananchi wana kila sababu ya kukichagua tena Chama Cha Mapinduzi kuendelea kuongoza nchi kwakuwa kinaahidi na kinatekeleza.

"Kuna watu wanazunguka kama mimi wakisema ilani zao, lakini kila nikiwasikiliza ni yaleyale yaliyopo kwenye ilani ya chama chetu, lakini ndani ya ilani ya Chama Cha Mapinduzi, tukiandika huku tukijua tutatekeleza kwa njia gani, fedha itatoka wapi, vipi tutakamilisha tuliyoyaandika. Suala siyo kusema tutafanya lakini vipi tutafanya hilo ndilo suala muhimu," ameeleza Dkt. Samia.

Ameongeza kuwa "CCM tunasimama na kujiamini kwa ujasiri mkubwa kuomba kura mtuchague tuendelee kuongoza serikali hii kwa sababu tumefanya nanyi mmeona na ninaamini tutafanya tena na mtaona".

Mbali ya kumsifu Dkt. Nchimbi ambaye ni mzaliwa wa Mkoa wa Ruvuma kuwa ana sifa za uongozi, Dkt. Samia ameahidi kuifungua Mikoa ya Kusini kuwa kitovu cha biashara na maendeleo.

Akiwa katika mikutano ya kampeni Songea Mjini, Namtumbo na Tunduru mgombea huyo ameainisha uwekezaji utakaofanywa na serikali yake katika kuchochea upatikanaji wa ajira kwa vijana.

Amesema katika hatua za maendeleo mikakati ya serikali yake ni kuufungua Mkoa wa Ruvuma na mingine ya Kusini kuwa kitovu cha biashara.

Amesema serikali yake itajenga kilometa 1,000 za reli ya kisasa itakayounganisha Mikoa yq Mtwara na Ruvuma na kurahisisha usafirishaji wa madini yatakayochimbwa Mchuchuma na Liganga.

Ameongeza kuwa, serikali yake itaboresha Kiwanja cha Ndege cha Songea na ujenzi wa Bandari ya Mbamba Bay ambao umefikia asilimia 35.

Pia amesema, serikali imekamilisha ujenzi wa Bandari ya Ndumbi ambayo imechochea biashara baina ya Tanzania na Malawi kupitia Nkata Bay hivyo kuongeza fursa za kiuchumi katika Ziwa Nyasa.

"Tunafungua ukanda wa kusini lengo likiwa biashara zifanyike kwa kutumia anga, barabara na maji ili Ruvuma iwe kitovu kikubwa cha biashara," ameeleza.

Dkt. Samia alisisitiza ahadi yake ya kukamilisha ujenzi wa barabara ya Kidatu - Ifakara - Malinyi hadi Lumecha inayounganisha Mikoa ya Ruvuma na Morogoro ambayo pia itachochea biashara.

Ameahidi kujenga na kukamilisha ujenzi wa Chuo Kikuu cha Uhasibu Arusha tawi la Songea na kujenga chuo cha ufundi cha walemavu Liganga.

Pia amesema serikali imetekeleza mradi wa ujenzi wa maghala 28 ya kuhifadhia mazao Mkoani Ruvuma.

Dkt. Samia ameahidi kuendeleza kutoa kipaumbele uchimbaji salama kwa wachimbaji wadogo.

Aidha amesema, wataendelea na mradi wa kuchimba madini ya Uranium na kuwa lengo la Serikali yake ni madini hayo yachakatwe na yasafishwe ndani ya nchi.

Pia ameahidi, kujenga barabara ya mchepuko kupunguza msongamano wa magari katikati ya mji wa Songea.

Leo Dkt. Samia anamalizia kampeni mkoani Ruvuma akiwa Nakapanya halafu anaingia Mtwara akianzia kampeni Nanyumbu na Masasi.

Na. Aboubakary Liongo - Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM

Chapisha Maoni

0 Maoni