Daraja la mawe Mto Katupa kukuza Sekta ya Kilimo Majimoto-Namanyele - Katavi

 

Ujenzi wa daraja la mawe katika Mto Katupa sambamba na barabara ya changarawe ya Majimoto-Namanyele katika Halmashauri ya Mpimbwe, mkoani Katavi, umetajwa kuwa mkombozi kwa wakulima wa eneo hilo, kwa kuongeza tija katika kilimo na kuchochea uchumi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa miradi hiyo, Meneja wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Mlele, Mhandisi Paul Mabaya alisema kuwa mradi huo unatekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 361.95 na hadi sasa umefikia asilimia 95 ya utekelezaji.

"Mradi huu unajumuisha ujenzi wa daraja la mawe, barabara ya changarawe yenye urefu wa kilomita 1.5 pamoja na kalvati tatu. Fedha za mradi huu zinatokana na ufadhili wa Benki ya Dunia kupitia mradi wa RISE," alisema Mhandisi Mabaya.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuboresha upatikanaji wa huduma muhimu kwa wananchi, hasa katika maeneo ya vijijini ambako shughuli za kilimo ndio mhimili mkuu wa uchumi wa wananchi.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2025, Ndugu Ismail Ali Ussi, alieleza kuwa serikali itaendelea kuhakikisha wananchi wake wanapata miundombinu bora ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

"Serikali kupitia miradi kama hii, inalenga kuweka mazingira wezeshi kwa wananchi wake. Hii ndiyo dhamira ya dhati ya kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika maendeleo," alisema Ussi.

Naye mkazi wa kijiji cha Majimoto, Shija Shigela, licha ya kuipongeza TARURA kwa ujenzi wa daraja na barabara hiyo, aliiomba mamlaka hiyo kuendelea na jitihada hizo kwa kujenga miradi mingine zaidi ya barabara vijijini.

"Miradi hii inatufungulia fursa nyingi, hasa sisi wakulima. Tunaiomba serikali na TARURA waendelee kutuunga mkono kwa kuboresha zaidi miundombinu ya barabara maeneo ya vijijini," alisema Shigela.

Miradi hii ni miongoni mwa hatua zinazochukuliwa na serikali katika kuhakikisha kuwa miundombinu ya usafiri vijijini inaimarika, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kupunguza umaskini na kuharakisha maendeleo ya wananchi katika ngazi ya chini.




Chapisha Maoni

0 Maoni