TMDA yabaini Dettol bandia sokoni, wageni wawili wakamatwa Kahama

 

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imebaini kuwepo kwa bidhaa bandia za maji ya Dettol zenye ujazo wa mililita 50, 125, 500 pamoja na lita moja, ambazo zimekuwa zikiuzwa katika soko la ndani kinyume na sheria.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, bidhaa hizo zimegundulika kupitia mifumo ya ukaguzi na ufuatiliaji wa bidhaa sokoni, na zimekuwa zikitengenezwa kwa njia isiyo halali huku zikiwa zimebandikwa lebo za kuonesha kuwa ni Dettol halisi.

TMDA imeeleza kuwa utengenezaji wa bidhaa hizo bandia ulibainika kufuatia taarifa za kiintelijensia zilizokusanywa na mamlaka hiyo, na baadaye kufuatiwa na ukaguzi uliofanyika kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi katika nyumba ya wageni ya New Kashinde Lodge iliyopo Mtaa wa Namanga, Kahama Mjini, mkoani Shinyanga.

Katika ukaguzi huo, walikuta vifaa mbalimbali vya kutengenezea bidhaa hizo ikiwa ni pamoja na kemikali, chupa tupu za Dettol, lebo, rangi, pamoja na madumu ya vimiminika. Vitu hivyo vilikuwa ndani ya chumba walichokuwa wanaishi raia wawili wa nchi jirani, ambao wanatuhumiwa kuhusika na tukio hilo.

Mamlaka hiyo imethibitisha kuwa watuhumiwa hao wamekamatwa na kufikishwa katika vyombo vya usalama, huku taratibu za kisheria za kuwafikisha mahakamani zikiendelea.

TMDA imetoa wito kwa wananchi kuwa makini na bidhaa wanazonunua sokoni, na kutoa taarifa kwa mamlaka husika endapo watabaini bidhaa zenye mashaka.

Chapisha Maoni

0 Maoni