SELF yatoa mikopo ya TZS bilioni 196.9, kwa wanufaika zaidi ya 183,000

 

Mfuko wa SELF (SELF Microfinance Fund) umefanikiwa kutoa mikopo yenye thamani ya Shilingi Bilioni 196.9 katika kipindi cha kuanzia mwaka 2021 hadi kufikia Juni 30, 2025, huku kiwango cha mikopo chechefu kikiripotiwa kuwa chini ya asilimia 10 na mfuko huo ukiweza kujiendesha kwa faida.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na uongozi wa mfuko huo jana kwa Wahariri wa Vyombo vya Habari, jumla ya wanufaika 183,381 wamefikiwa na mikopo hiyo, ambapo wanawake walikuwa 97,170 sawa na asilimia 53 na wanaume 86,211 wakichangia asilimia 47 ya wanufaika wote.

Katika kipindi hicho, SELF pia imefanikiwa kuzikopesha na kuzijengea uwezo taasisi ndogo za fedha 549, hatua inayolenga kuboresha huduma na ufanisi katika sekta ya huduma ndogo za kifedha nchini.

“Kuziwezesha taasisi hizi kwa maarifa na mbinu bora za uendeshaji kumechangia kupunguza changamoto mbalimbali katika utoaji wa huduma kwa jamii,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Aidha, mfuko huo umechangia kwa kiasi kikubwa katika uundaji wa ajira, ambapo zaidi ya nafasi 183,000 za ajira zimeripotiwa kutengenezwa kupitia wakopaji na shughuli wanazozifanya kuanzia mwaka 2021 hadi Juni 2025.

Katika jitihada za kuchochea maendeleo endelevu na kulinda mazingira, SELF imeanza pia kutoa mikopo kwa ajili ya upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuhamasisha matumizi ya nishati mbadala kwa kaya mbalimbali.

Mbali na hayo, SELF imeendesha mafunzo ya elimu ya fedha kwa wananchi 10,378 katika kipindi hicho, ikiwa ni mkakati wa kuinua uelewa wa jamii kuhusu masuala ya kifedha, usimamizi wa mikopo na ujasiriamali.

Chapisha Maoni

0 Maoni