The Same Quality Foundation yaendesha kambi ya upasuaji wa midomo wazi Zanzibar

 

Taasisi ya The Same Quality Foundation inayopatikana Arusha, kwa kushirikiana na Wizara ya Afya pamoja na Hospitali ya Lumumba ya Zanzibar, imeendesha kambi ya upasuaji wa midomo wazi kwa watu wenye tatizo hilo, ikiwa ni muendelezo wa huduma zinazotolewa na taasisi hiyo kwa lengo la kuhakikisha watoto na watu wenye midomo wazi wanapatiwa matibabu.

Akizungumza kuhusu kambi hiyo, Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Dkt. Piter Mabula, amesema tangu waanze kushirikiana na sekta ya afya nchini Tanzania, tayari wameweza kutoa matibabu kwa zaidi ya watu 2,500, ambapo kati yao, 200 wamehudumiwa hapa Zanzibar.

Dkt. Mabula ameongeza kuwa kwa wiki moja, wataalamu wa taasisi hiyo watakuwa katika Hospitali ya Lumumba wakifanya upasuaji kwa kushirikiana na baadhi ya madaktari bingwa wa ndani ya nchi, ili kuhakikisha huduma hiyo inawafikia wahitaji wengi zaidi.

Amesisitiza kuwa huduma hizi hazitozwi malipo yoyote, na ametoa wito kwa jamii, hasa wazazi wa watoto wenye tatizo la midomo wazi, kuwafikisha hospitalini mapema ili waweze kupata matibabu. Ameeleza kuwa taasisi yao imejipanga kusaidia jamii na kuondoa changamoto ya tatizo hilo kwa watoto na watu wazima.

Aidha, Dkt. Mabula ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya kwa ushirikiano mkubwa waliouonesha katika miaka 11 ya utekelezaji wa huduma hizi kwenye hospitali mbalimbali za Unguja na Pemba, zikiwemo Hospitali ya Abdalla Mzee mkoani na Mnazi Mmoja.

Kwa upande wake, Daktari wa kinywa na meno kutoka Hospitali ya Lumumba, Dkt. Sumaiyya Said Aboud, amesema kambi hizo ni endelevu na hufanyika mara mbili kwa mwaka, ambapo kwa sasa wanatarajia kufanya upasuaji kwa watoto 25. Amesisitiza kuwa wazazi wawapeleke watoto hospitalini mapema ili wapate huduma na kuishi maisha ya kawaida.

Ameeleza kuwa tatizo la midomo wazi linaweza kuondolewa kabisa kupitia upasuaji, na kwamba linapomkumba mtoto huathiri muonekano wake, uwezo wa kula, na hata kuzungumza. Hivyo, amewataka wazazi kuwa na mwitikio wa haraka kufikisha watoto wao hospitalini ili wapewe matibabu.

Naye Bi Leyla Saidi, mzazi wa mtoto aliyefika hospitalini kwa ajili ya matibabu, amesema mtoto wake anaendelea vizuri na sasa anaweza kuzungumza kwa ufasaha. Amewahamasisha wazazi wenye watoto wenye matatizo kama hayo kupeleka watoto wao hospitalini kwa kuwa huduma hutolewa kwa weledi na bila usumbufu wowote.

Wananchi waliopatiwa huduma na taasisi hiyo wamesema wamefurahishwa na huduma bora walizopokea na wameipongeza taasisi kwa moyo wa kutoa misaada ya afya, wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kuunga mkono juhudi hizo kwa ustawi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

The Same Quality Foundation inaendelea kutoa huduma mbalimbali za afya kwa jamii ya Tanzania Bara na Zanzibar, kwa kuwalenga hasa watoto na watu wazima wenye matatizo ya midomo wazi. Kwa sasa, huduma hizo zinaendelea kutolewa hapa Zanzibar kwa muda wa wiki moja.



Chapisha Maoni

0 Maoni