TCRA yawafunda Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni kuelekea Uchaguzi Mkuu

 

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewaasa wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni kutotoa taarifa ambazo zitaleta taharuki na machafuko ndani ya nchi hasa katika kuelekea kipindi cha Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakao fanyika baadaye mwaka huu.

Hayo yamesemwa jana  Agosti 3, 2025 na Meneja Kitengo cha Huduma za Utangazaji, TCRA, Injinia Andrew Kisaka wakati  akiwasilisha makala (mada) katika mkutano ulioandaliwa na  wa  Tume Huru ya Uchaguzi nchini (INEC) kwa  watoa maudhui mtandaoni, amesema kuwa wakati wa uchaguzi kuna mazingira ya migawanyiko, mivutano ya kijamii, na upotoshaji wa hali ya juu hivyo ni muhimu kuepuka kusambaza uvumi, kuripoti kwa umakini, kutopendelea upande wowote  na kukemea lugha za chuki.

Kisaka amewataka wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni nchini kote kuimarisha maadili yao na kuchukua jukumu muhimu katika kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani kwa kupandisha maudhui yenye tija na kama unaona maudhui yataleta taharuki  ni bora kuachana nayo.

Aidha, Kisaka ametoa mfano wa  Historia ya machafuko ya uchaguzi yaliyotea katika nchi Kenya  (2007) na Nigeria (2011), amesema kuwa katika machafuko hayo zaidi ya watu 800 walipoteza uhai nchini Nigeria mwaka 2011 wakati nchini Kenya zaidi ya watu 1,000 walipoteza uhai na wengine 600,000 kupoteza makazi.

Aidha, amesema kuwa  katika mazingira magumu yenye shinikizo la juu la uchaguzi, vyombo vya habari vinaweza kujikuta vikichangia machafuko kwa kueneza uvumi au kuchochea upendeleo wa kisiasa.

Amesema ili kukabiliana na maafa wakati wa uchaguzi na baada kuna miongozo ya kuripoti ambayo inatatua changamoto hizo.

"Uvumi ndiyo chanzo kikuu cha vurugu hivyo  vyombo vya habari vinapaswa kuchunguza kwa kina uvumi na kutoa taarifa sahihi haraka iwezekanavyo ili kuzuia mzunguko wa vurugu za kulipiza kisasi." amesema Mhandisi Kisaka.

Pia amehimiza waandaaji wa Maudhui Mitandaoni wakiwamo Mabloga kukataa lugha na vichwa vya habari vya kichochezi.

"Msiripoti kila kauli ya uchochezi kutoka kwa wanasiasa, hata kama kauli hizo zinaonekana kuwa habari kwenu na zenye kuvutia msomaji acha kabisa ni muhimu kutokuzirudia kwenye vichwa vya habari, " amesema Mhandisi Kisaka na kuongeza kuwa lugha inayodhalilisha inaweza kuchochea wananchi kutenda vitendo vya kikatili.

Aidha, amesema kuwa  katika kipindi hiki cha uchaguzi, ni  vyema wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni kuchukua tahadhari binafsi  kutoa  matangazo ya moja kwa moja 'live'   ya mikutano ya kampeni za wagombea kwa sababu yanaweza leta  machafuko.

"Matangazo ya moja kwa moja 'live'  ya machafuko ya uchaguzi yanatakiwa kufanywa na Waandishi Waandamizi na  wenye  uzoefu na siyo 'One Man Show' kama ilivyo kwa baadhi ya wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni.

Wanaohamasisha chuki na vurugu hawapaswi kupewa nafasi hewani," amesema Mhandisi Kisaka.

Aidha, amesema kuwa  vyombo vya habari vinapaswa kuzuia kuonesha picha zinazochochea vurugu  na ikiwa  ni lazima, kusimamisha matangazo ya moja kwa moja ili kuzuia hali kuwa mbaya zaidi.

Maafa na miongozo ya kuripoti katika hali ambapo uchaguzi unafanyika wakati wa maafa, ni sehemu ya elimu zinazotolewa kwa  wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni katika kuhakikisha taifa linavuka salama katika uchaguzi wa mwaka 2025 kama ilivyokuwa katika chaguzi nyingine.

Chapisha Maoni

0 Maoni