Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila,
amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, imejipanga kwa dhati kuendeleza
michezo nchini kwa kuweka mazingira bora ya mafanikio kwa vijana.
Akizungumza leo Agosti 22, 2025 jijini Dar es Salaam katika
mkutano na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya mchezo wa kuwania kufuzu
CHAN kati ya Taifa Stars na Morocco, Mhe. Chalamila alibainisha kuwa Rais Samia
ameidhinisha zawadi ya viwanja kwa wachezaji wa Taifa Stars katika eneo la
Kigamboni pamoja na shilingi milioni 20 taslimu, kama sehemu ya kutambua
mchango wao kwa taifa.
“Hii zawadi ya viwanja na shilingi milioni ishirini
haitahusishwa na matokeo ya mchezo. Iwe tumeshinda au tumepoteza, vijana wetu
wa Taifa Stars watapata zawadi hizi kwa kutambua mchango wao na kuwatia moyo
zaidi,” alisema Chalamila.
Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza kuwa serikali imejipanga
kuhamasisha na kuwaunga mkono vijana wanaoiwakilisha nchi katika ngazi ya
kimataifa, akieleza kuwa kwa kila bao litakalofungwa na Taifa Stars kwenye
mchezo huo, serikali itatoa motisha ya shilingi milioni tano.
“Kila goli litakaloingia wavuni kutoka kwa vijana wetu wa
Taifa Stars, serikali itachangia shilingi milioni tano kama sehemu ya kuwatia
moyo,” alisema.
Kwa mujibu wa Chalamila, hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za
serikali kuongeza morali kwa wachezaji na kuonyesha mshikamano wa dhati kati ya
serikali, wananchi na timu ya taifa katika mashindano ya kimataifa.
“Hii ni sehemu ya mikakati ya Mheshimiwa Rais kuhakikisha
michezo inakuwa na vijana wetu wanathaminiwa ipasavyo. Tunatoa rai kwa wadau wa
michezo kujitokeza na kuunga mkono jitihada hizi za kuinua soka letu,”
aliongeza Chalamila.
Mchezo huo ni sehemu ya hatua muhimu kwa Tanzania kuelekea kushiriki michuano ya Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani (CHAN), na serikali imeahidi kuendelea kuboresha mazingira ya michezo ili kufikia mafanikio ya muda mrefu.
0 Maoni