Kituo cha Kisasa cha Kuchakata Asali Chanzinduliwa Kahama

 

Wakulima wa nyuki katika Kijiji cha Kangeme, Kata ya Ulowa, wilayani Kahama sasa wanatarajia kunufaika na ongezeko la thamani ya mazao ya nyuki baada ya kuzinduliwa kwa kituo cha kukusanya na kuchakata asali kilichojengwa kwa gharama ya Sh milioni 84.

Kituo hicho, chenye uwezo wa kuhifadhi zaidi ya tani 90 za asali, kimejengwa na Shirika la Maendeleo la Ubelgiji (Enabel) chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) chini ya mradi wa BEVAC.

Akizindua kituo hicho kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mkuu wa Wilaya ya Kahama Frank John Mkinda alisisitiza usimamizi makini wa mradi huo ili kuhakikisha unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wanachama na jamii kwa ujumla.

“Ninawataka viongozi wa Chama cha Ushirika cha Wafugaji Nyuki Ulowa kuhakikisha kituo hiki kinasimamiwa vizuri na kufikia malengo yaliyowekwa. Hii ni fursa kubwa ya kuongeza kipato kwa wananchi,” alisema.

Vilevile, aliitaka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kushirikiana kwa karibu na wafugaji nyuki hao kwa kuwajengea uwezo, kuwasaidia kuongeza tija katika uzalishaji na kuhakikisha wanapata masoko yenye uhakika.

Mbali na hayo, alihimiza washiriki wote kuimarisha uwezeshaji katika mavuno ya mazao yatokanayo na nyuki ili kuongeza thamani na usalama wa kipato cha wananchi.

Mara baada ya hotuba hiyo, Mkuu wa Wilaya alifungua kituo hicho na kukabidhi rasmi nyaraka za umiliki kwa Chama cha Wafugaji Nyuki Ulowa, ambacho sasa kitakuwa msimamizi na mmiliki halali wa kituo hicho.



Chapisha Maoni

0 Maoni