Bidhaa zitokanazo na Mazao ya Misitu zawa kivutio Maonesho ya Nane Nane

 

Wananchi mbalimbali wameendelea kutembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii ili kujionea, kujifunza na kununua bidhaa mbalimbali ambazo zinatokana na mazao ya misitu katika Maonesho ya Nane Nane Jijini Dodoma.

Wananchi wanatembelea sehemu ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania na kuona bidhaa hizo ikiwa ni pamoja na thamani mbalimbali zitokanazo na miti, mianzi na kamba za porini (hezilani) ambazo zimetumika kutengeneza thamanj hizo.

Wananchi hao wamevutiwa na ubora na uzuri wa bidhaa hizo ambazo zinatengenezwa hapa nchini kutokana na mazao mbalimbali yatokanayo na misitu ikiwa ni pamoja na viti, vitanda, mapambo  na thamani nyingi mbalimbali.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao wamesema kuwa wamekuwa wakiona thamani kama hizo zikitoka nje ya nchi na kwasasa zinazalishwa hapa Tanzania kwa ubora wa hali ya juu.

"Kwa sasa tunajivunia kuwa na bidhaa zetu wenyewe ambazo zinazalishwa hapahapa nchini na nimeona kwa kweli zina ubora wa hali juu na bei zake ni nafuu sana," amesema Teddy Masanja.

Mbali na bidhaa na upatikanaji wa bidhaa hizo, Wataalamu kutoka TFS  wanaendelea kutoa elimu ya miche na upatikanaji wa mbegu bora za miti , fursa ya kujionea shughuli za ufugaji nyuki, zikiwemo maandalizi ya manzuki, uvunaji na uchakataji wa mazao ya nyuki na bidhaa zake

Aidha, TFS imewahimiza wananchi kuendelea kutembelea banda lao katika maonesho ya NaneNane ambayo yanafanyika Viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma na katika maeneo mengine nchini yanapofanyika Kikanda ili kupata elimu zaidi juu ya uhifadhi wa misitu, ufugaji wa nyuki, pamoja na kupata ofa maalumu za kutembelea vivutio vya utalii wa ikolojia vinavyosimamiwa na wakala huo.

Maonesho ya Nane Nane yameanza Agosti 1,2025 na yanatarajiwa kufika kilele chake Agosti 8,2025 yenye kauli mbiu " Chagua Viongozi Bora kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi 2025".




Chapisha Maoni

0 Maoni