Wataalamu wabainisha chanzo cha kuongezeka kwa visa vya saratani ya ini

 

Saratani ya ini iko katika njia ya kuwa janga kubwa zaidi la kiafya duniani, hasa kwa watu wazima wa umri mdogo, huku visa vya ugonjwa huo vikitarajiwa kuongezeka maradufu kufikia mwaka 2050, wataalamu wameonya.

Awali saratani ya ini ilionekana kuwa ugonjwa unaowakumba zaidi wazee waliokuwa na maambukizi ya homa ya ini (hepatitis) au utegemezi wa pombe. Hata hivyo, kwa sasa ugonjwa huu unazidi kugundulika kwa watu wenye umri wa miaka 30 na 40.

Uchambuzi mkubwa mpya uliochapishwa kwenye jarida la The Lancet umehusisha mabadiliko haya na kuongezeka kwa unene wa kupindukia (obesity) pamoja na magonjwa yanayohusiana na ini kama vile MASLD (ugonjwa wa ini unaohusiana na hitilafu ya kimetaboliki na mafuta kwenye ini).

Ripoti hiyo inakadiria kuwa idadi ya visa vipya vya saratani ya ini duniani itaongezeka kutoka visa 870,000 mnamo 2022 hadi kufikia milioni 1.52 ifikapo mwaka 2050. Vifo vya kila mwaka kutokana na ugonjwa huo vinatarajiwa kuongezeka kutoka 760,000 hadi milioni 1.37 katika kipindi hicho.

Wataalamu wanasema kwamba mojawapo ya visababishi vinavyoongezeka kwa kasi ni MASH (aina kali ya MASLD), hali mbaya ya ugonjwa wa ini yenye mafuta inayohusishwa na unene wa kupindukia na matatizo ya kimetaboliki.

Idadi ya saratani ya ini inayosababishwa na MASH inatarajiwa kuongezeka zaidi ya mara mbili – kutoka asilimia 5 mwaka 2022 hadi asilimia 11 mwaka 2050.

Wakati huohuo, idadi ya visa vinavyosababishwa na virusi vya hepatitis B – ambavyo kwa sasa ndiyo chanzo kikuu cha saratani ya ini – inatarajiwa kupungua. Vivyo hivyo, visa vinavyosababishwa na virusi vya hepatitis C navyo vinakadiriwa kupungua kwa kiasi fulani.

Hata hivyo, idadi ya visa vinavyotokana na unene wa kupindukia na unywaji pombe inatarajiwa kuongezeka katika kipindi hicho hicho.

Kufikia mwaka 2050, zaidi ya robo ya visa vya saratani ya ini vitasababishwa na pombe, na kimoja kati ya kila visa kumi kitasababishwa na aina kali ya MASLD, ambayo zamani ilijulikana kama ugonjwa wa ini lenye mafuta.

Hali hiyo hutokea pale mafuta yanapokusanyika kwenye ini la mtu, na inahusishwa sana na unene wa kupindukia na ugonjwa wa kisukari aina ya pili.

Timu ya watafiti kutoka Hong Kong imebainisha kuwa asilimia 60 ya visa vya ugonjwa huu hatari vinaweza kuzuilika.

Kuhusu matokeo ya utafiti huo, watafiti wamesema yanadhihirisha haja ya kuchukua hatua za kinga dhidi ya saratani ya ini, inayojulikana pia kama hepatoselula kansa (hepatocellular carcinoma).

Matibabu makuu ya MASLD ni kula lishe bora, kuwa na shughuli za mwili mara kwa mara, na inapobidi kupunguza uzito.

“Saratani ya ini ni tatizo linalozidi kuwa kubwa kiafya duniani,” alisema Profesa Jian Zhou, Mwenyekiti wa Kamisheni hiyo kutoka Chuo Kikuu cha Fudan, China.

Chapisha Maoni

0 Maoni