Trump kusitisha misaada kusababisha vifo zaidi ya milioni 14

 

Hatua ya Donald Trump ya kupunguza kwa kiasi kikubwa ufadhili wa Marekani kwa misaada ya kibinadamu inaweza kusababisha vifo vya ziada zaidi ya milioni 14 kufikia mwaka 2030, kwa mujibu wa utafiti uliochapishwa katika jarida la kitabibu la The Lancet.

Utafiti huo unaonesha kuwa theluthi moja ya waliopo hatarini kufa mapema ni watoto.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, alisema mwezi Machi kuwa serikali ya Rais Trump ilikuwa imefuta zaidi ya asilimia 80 ya mipango yote ya Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).

Kwa mujibu wa Davide Rasella, mmoja wa waandishi wa ripoti hiyo kutoka The Lancet, "Kwa nchi nyingi za kipato cha chini na cha kati, mshtuko utakaotokana na hatua hii utalingana na athari za janga la dunia au machafuko ya kivita."

Rasella, ambaye pia ni mtafiti katika Taasisi ya Afya ya Kimataifa ya Barcelona, aliongeza kuwa kupunguzwa kwa ufadhili huo "kunahatarisha kusitisha ghafla na kurudisha nyuma mafanikio ya miongo miwili katika afya ya jamii zilizo hatarini."

Ripoti hii inachapishwa wakati viongozi kadhaa wa dunia wanakutana katika jiji la Seville, Hispania, kwa ajili ya mkutano wa misaada unaoongozwa na Umoja wa Mataifa,mkutano mkubwa zaidi wa aina yake katika kipindi cha miaka kumi.

Kwa kuangalia data kutoka nchi 133, timu ya watafiti ilikadiria kuwa ufadhili wa USAID ulisaidia kuzuia vifo milioni 91 katika nchi zinazoendelea kati ya mwaka 2001 na 2021.



Chapisha Maoni

0 Maoni