Wananchi wamehimizwa
kuchangamkia fursa ya kufanya biashara ya mazao ya nyuki kufuatia elimu
iliyotolewa jana Julai 8, 2025 na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS)
katika banda lao lililopo ndani ya banda la Wizara ya Maliasili na Utalii.
Akizungumza wakati
akitoa elimu hiyo, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Grace Buchukundi, alisema
biashara ya mazao ya nyuki ni moja ya sekta zenye fursa kubwa lakini bado
wananchi wengi hawana taarifa sahihi za kisheria na kiutendaji kuhusu namna ya
kuingia sokoni.
“Sheria ya Ufugaji
Nyuki Na.15 ya mwaka 2002 na Kanuni zake za mwaka 2005 zimeweka misingi ya
usimamizi wa ubora na usalama wa mazao ya nyuki. Kila mfugaji au mfanyabiashara
anatakiwa kusajiliwa katika Ofisi za TFS za Wilaya husika,” alisema Buchukundi.
Mmoja wa wananchi
waliotembelea banda hilo, Mohamed Juma, alisema elimu hiyo imemfungua macho
baada ya muda mrefu kutamani kuingia kwenye biashara ya mazao ya nyuki bila
kufahamu hatua zinazohitajika.
“Nimepata kuelewa
kuwa ili kuanza, lazima uwe na nyaraka muhimu kama leseni kutoka BRELA,
kitambulisho cha Taifa (NIDA), hati ya mlipa kodi (TRA) na muhtasari wa kampuni
kwa wale wenye kampuni. Pia kuna ada ya usajili ya Shilingi 53,000 kwa mwaka na
gharama za ukaguzi wa ubora,” alisema.
Kwa mujibu wa Buchukundi,
wafanyabiashara wa ndani na wale wanaokusudia kuuza asali na nta nje ya nchi
wanatakiwa pia kulipia ada za vibali na usafi kulingana na uzito wa shehena.
Ada za kuuza nje huanzia Shilingi 110,000 kwa mwaka mmoja wa kiserikali.
Akitoa wito kwa umma,
TFS imewataka wananchi kufika katika banda lao kupata elimu zaidi pamoja na
kununua Misitu Honey, asali safi na bora inayozalishwa na Wakala huo. Aidha,
wananchi wanahimizwa kununua miche na mbegu bora za miti ili kuchangia uhifadhi
wa misitu na ustawi wa mazingira.
“Tunakaribisha
wananchi waje kujipatia asali yenye ubora na miche bora kwa bei nafuu. Lengo
letu ni kuhakikisha jamii inanufaika na rasilimali za misitu kwa njia
endelevu,” aliongeza Buchukundi.
Maonesho hayo
yanatarajiwa kuendelea hadi mwishoni mwa wiki hii huku wananchi wakihimizwa
kuchangamkia fursa zilizopo.
0 Maoni