Binti wa Rais Museveni avunja ndoa, sasa yupo single

 

Hatimaye binti wa Rais wa Uganda Yoweri Kaguta Museveni, Diana Kamuntu, ametangaza rasmi kuwa yuko single, baada ya ndoa yake ya miaka 18 kuvunjika kisheria.

Diana, ambaye alizaliwa mwaka 1980, ni mtoto wa pili wa Rais Museveni na Mkewe Janet Kataaha Museveni. Alifunga ndoa na mfanyabiashara Geoffrey Kamuntu tarehe 24 Julai 2004, ndoa ambayo ilijaliwa watoto watatu, wavulana wawili na msichana mmoja.

Kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa, Mahakama ilitoa uamuzi wa kuvunjika kwa ndoa hiyo mnamo mwaka 2022 kupitia amri ya kisheria ya Decree Nisi, ambayo huashiria hatua ya awali ya talaka kabla ya kuwa rasmi (Decree Absolute).

Katika hatua ya hivi karibuni, Diana ametangaza kuachana rasmi na jina la ukoo wa aliyekuwa mumewe, “Kamuntu”, na kurejea kutumia jina la familia ya mzazi wake, sasa akijitambulisha kama Diana Museveni Kyaremera.

Ingawa sababu za kuvunjika kwa ndoa hiyo hazijawekwa wazi, vyanzo vya karibu vinaeleza kuwa wawili hao walikuwa na tofauti zisizoweza kupatanishwa kwa muda mrefu.

Wakati familia ya Museveni kwa kawaida huepuka kuweka maisha yao binafsi wazi kwa umma, hatua ya Diana kutangaza hali yake ya ndoa imezua mjadala mkubwa kwenye mitandao ya kijamii, huku wengi wakitoa maoni mbalimbali kuhusu uamuzi huo.

Hadi sasa, upande wa Geoffrey Kamuntu haujatoa kauli yoyote rasmi kuhusu suala hilo.

Chapisha Maoni

0 Maoni