Serikali yakanusha tuhuma za mpango wa kumwekea Lissu

 

Serikali ya Tanzania imekanusha vikali tuhuma zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii zinazodai kuwa kuna mpango wa kumwekea sumu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Antipas Lissu, ambaye kwa sasa anakabiliwa na kesi mahakamani.

Kupitia taarifa iliyotolewa leo na Idara ya Habari (MAELEZO), Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, amesema tuhuma hizo hazina msingi wowote na kwamba Serikali haina mpango wala dhamira ya kufanya jambo la namna hiyo.

"Serikali inawaomba wananchi kupuuza taarifa hizo kwa kuwa si za kweli na zinalenga kupotosha umma," alisema Msigwa katika taarifa hiyo.

Amefafanua kuwa Lissu, ambaye ametajwa kwenye taarifa hizo pamoja na kauli za baadhi ya wanasiasa wa nje ya nchi, kwa sasa yupo gerezani kwa mujibu wa sheria, akisubiri shauri lake kukamilika mahakamani.

Msemaji huyo amesisitiza kuwa Serikali haijawahi kuwa na mpango wa kumuwekea sumu mfungwa yeyote na wala haina nia ya kufanya hivyo kwa mtu yeyote anayeendelea kushikiliwa kwa mujibu wa sheria.

Amesema kusambazwa kwa taarifa hizo ni sehemu ya njama za kuharibu taswira ya nchi kimataifa na kuchafua heshima ya Tanzania, ambayo imejijengea sifa ya kuheshimu haki, sheria na taratibu.

"Tayari mamlaka zinazohusika zimeanza kuchukua hatua dhidi ya wote waliohusika kuchapisha na kusambaza uongo huu," imeeleza taarifa hiyo.

Serikali imetoa wito kwa wananchi kuwa na subira na kuendelea kuiamini mifumo rasmi ya utoaji wa taarifa huku ikiweka wazi kuwa haitavumilia upotoshaji unaolenga kuchochea hofu au kuleta taharuki kwa jamii.



Chapisha Maoni

0 Maoni