CCM kuanza mchakato wa mchujo wa wagombea kesho

 

Baada ya kukamilika kwa zoezi la uchukuaji na urejeshaji wa fomu za kuwania nafasi za ubunge na udiwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), sasa mchakato unahamia katika hatua nyingine muhimu ya kuchambua na kupendekeza majina ya wagombea.

Kuanzia kesho, Julai 4, 2025, kamati za siasa katika ngazi mbalimbali zinaanza vikao maalumu kwa ajili ya kuwajadili wanachama waliotia nia ya kugombea nafasi hizo, kabla ya kupitishwa kwa majina ya mwisho katika ngazi ya taifa.

Kwa mujibu wa ratiba rasmi iliyotolewa na CCM, vikao vya kamati za siasa za kata na wadi vitaanza kesho kwa ajili ya kuwajadili wagombea wa nafasi ya udiwani wa kawaida pamoja na wa viti maalumu. Baada ya uchambuzi huo, mapendekezo yatapelekwa kwenye kamati za siasa za ngazi ya jimbo kwa upande wa Zanzibar na wilaya kwa upande wa Tanzania Bara.

Vikao hivyo vitaendelea Julai 5, 2025, ambapo kamati za siasa za majimbo kwa upande wa Zanzibar zitawajadili wagombea wa nafasi za udiwani, ubunge na uwakilishi. Mapendekezo ya vikao hivyo yatapelekwa kwa kamati za siasa za wilaya kwa hatua zaidi.

Hatua hii ni sehemu ya mchakato mpana wa ndani wa chama unaolenga kuhakikisha upatikaji wa wagombea wenye sifa, uadilifu na uwezo wa kuwatumikia wananchi kwa ufanisi.

Chapisha Maoni

0 Maoni