Jeshi la Polisi
mkoani Mbeya linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kupanga njama ya kumuua
mama yao mzazi kwa imani za kishirikina, katika tukio ambalo pia mtoto mwenye
umri wa miaka minne alijeruhiwa kwa risasi. Aidha, mtuhumiwa mmoja wa tukio
hilo ameuawa kwa kupigwa risasi wakati wa mapambano na polisi.
Akizungumza na
waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, SACP Benjamini Kuzaga,
amesema tukio hilo lilitokea usiku wa Juni 13, 2025, majira ya saa 6:05 katika
Kijiji cha Ipwizi, Kata ya Mjele, Wilaya ya Mbeya Vijijini.
Kamanda Kuzaga
alieleza kuwa katika tukio hilo, mtoto aitwaye Sinzo Jifwalo (4), alijeruhiwa kwa
risasi za shotgun begani na mdomoni akiwa amelala ndani ya chumba pamoja na
bibi yake, Bi. Kweji Lugembe (75), ambaye ndiye alilengwa kuuawa.
Taarifa za awali
zinaonesha kuwa tukio hili linahusishwa na imani za kishirikina ambapo watoto
wa Bi. Kweji waliwahi kumtuhumu mama yao kuwa anajihusisha na ushirikina
unaodaiwa kusababisha vifo vya baadhi ya watoto wa familia hiyo,” alisema
Kamanda Kuzaga.
Watuhumiwa wakuu wa
tukio hilo ni Seven Kipara (38) na mdogo wake Jifaru Kipara, ambao wanadaiwa
kupanga njama ya mauaji kwa kumkodi mtu anayejulikana kwa jina la Tabi Deus
(39), mkazi wa Kilwa Masoko – Lindi, kwa makubaliano ya kumlipa shilingi
milioni tano. Tabi Deus aliandamana na mshirika wake anayefahamika kwa jina la
Shija.
Kwa mujibu wa taarifa
ya polisi, mnamo Juni 8, Tabi Deus na Shija walifika Mji Mdogo wa Mbalizi
ambako walipokelewa na Seven Kipara na kisha kufikishwa katika eneo la tukio.
Juni 13 usiku, Deus alifyatua risasi mbili kupitia dirishani akiwa na lengo la
kumuua Bi. Kweji, lakini risasi hizo zilimpata mtoto mdogo aliyejeruhiwa
vibaya.
Polisi walifanikiwa
kuwakamata Tabi Deus na Seven Kipara, ambapo Deus alikutwa na bastola ya
kutengenezwa kienyeji isiyo na namba pamoja na risasi mbili za shotgun ndani ya
mkoba.
Mnamo Juni 15, saa
1:00 jioni, Tabi Deus aliwaongoza polisi hadi maficho ya mshirika wake Shija
pamoja na silaha. Hata hivyo, Shija alipoona askari, alijaribu kukimbia na
kuwapuuza walipomwamuru asimame. Polisi walifyatua risasi tatu hewani, lakini
Shija aliendelea kukimbia ndipo alipolengwa na kupigwa risasi mguuni.
Alikimbizwa katika Hospitali Teule ya Ifisi ambako alifariki dunia wakati
akipatiwa matibabu.
Kamanda Kuzaga
amesema kuwa msako wa kuwatafuta watuhumiwa wengine unaendelea, na ametumia
nafasi hiyo kuwaonya wote wanaojihusisha na vitendo vya kishirikina na mauaji
kuwa sheria haitasita kuchukua mkondo wake.
“Jeshi la Polisi Mkoa
wa Mbeya linaendelea na msako wa watuhumiwa waliobakia na tunatoa onyo kali kwa
yeyote anayehusika na vitendo vya kishirikina – sheria itachukua mkondo wake
bila muhali,” amesema Kamanda.
Jeshi la Polisi pia
limewaasa wananchi kuachana na imani potofu na kutafuta suluhisho la migogoro
kupitia njia za kisheria badala ya kujichukulia sheria mikononi.
0 Maoni