Jeshi la Polisi Mkoa
wa Mbeya linamshikilia mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Sayansi
na Teknolojia Mbeya (MUST), Emilian Joseph Duzu (21) kwa tuhuma za kumuua kwa
kumchoma na kitu chenye ncha kali mwanafunzi mwenzake wa mwaka wa tatu, Gerald
Philbert Said (22).
Tukio hilo lilitokea
alfajiri ya Juni 14, 2025, majira ya saa 11:00, katika klabu moja inayojulikana
kama Mbeya Pazuri, iliyopo Jijini Mbeya.
Akithibitisha tukio
hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, SACP Benjamini Kuzaga, amesema kuwa
mtuhumiwa Emilian Duzu anadaiwa kumchoma marehemu Gerald Philbert Said tumboni
kwa kutumia kitu chenye ncha kali, hali iliyosababisha majeraha makubwa.
“Baada ya tukio hilo,
marehemu alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya kwa matibabu,
lakini alifariki dunia majira ya saa 7:00 mchana siku hiyo hiyo,” alisema SACP
Kuzaga.
Kwa mujibu wa Kamanda
huyo, uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo ni ugomvi
uliosababishwa na ulevi wa kupindukia. Inadaiwa kuwa wawili hao walikuwa
wakibishana ndani ya klabu hiyo, na walinzi (mabaunsa) waliamuru watoke nje.
Hapo ndipo mtuhumiwa alielekea kwenye gari lake alikokuwa ameegesha nje, na
marehemu alimfuata kwa lengo la kuendeleza ugomvi huo, ndipo akachomwa na kitu
chenye ncha kali.
Kamanda Kuzaga ametoa
wito kwa wananchi, hususan vijana na wanafunzi wa vyuo vikuu, kuzingatia
maadili, kujiepusha na ulevi wa kupindukia na kutatua tofauti zao kwa njia ya
amani.
“Vitendo vya uhalifu
havina nafasi katika jamii. Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya litaendelea kuchukua
hatua kali kwa mujibu wa sheria kwa yeyote atakayejihusisha na vitendo vya
namna hii,” amesisitiza Kamanda Kuzaga.
Mtuhumiwa
anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa hatua zaidi za kisheria, huku uchunguzi
ukiendelea.
0 Maoni